The House of Favourite Newspapers

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 35

0

ILIPOISHIA:

Harakaharaka tukatoka na kuingia ndani ya teksi, safari ya kurudi hospitalini ikaanza huku muda wote Shamila akiwa na furaha ya ajabu, akawa ananimwagia mvua ya mabusu. Dakika kadhaa baadaye, tuliwasili hospitalini lakini mazingira ya pale yalinishtua mno, hofu kubwa ikaukumba moyo wangu tulipofika kwenye maegesho ya magari.

SASA ENDELEA…

Gari jeusi lililokuwa na vioo vya rangi nyeusi (tinted), Isuzu Bighorn lilikuwa limepaki kwenye maegesho hayo huku milango ya upande mmoja ikiwa wazi. Kumbukumbu zangu zilionesha kwamba hiyo haikuwa mara ya kwanza kuliona gari hilo machoni mwangu, nikawa najaribu kukumbuka ni wapi?

Shamila alimlipa dereva teksi na kutaka kushuka lakini nikamzuia, akabaki anashangaa. Niliendelea kulitazama lile gari na kwa makini, ghafla kengele ya hatari ikalia ndani ya kichwa changu baada ya kumuona mmoja kati ya watu waliokuwa ndani ya gari hilo.

Alikuwa ni kijana mmoja mwenye asili ya Bara la Asia, ambaye rangi ya ngozi yake ilikuwa ikifanana sana na ya Shenaiza pamoja na mdogo wake, kuonesha kwamba walikuwa na aina fulani ya unasaba kati yao. Nilipozidi kumtazama, nilimkumbuka kwamba mimi na yeye tulikutana kwenye matukio mawili tofauti, tena yote ya hatari yakimhusisha Shenaiza.

Tukio la kwanza lilikuwa ni siku nilipokuwa najaribu kumtorosha Shenaiza hospitalini, kipindi hicho wakati ndiyo kwanza tumeanza kufahamiana. Tukio la pili, ambalo liliyafanya mapigo ya moyo wangu yaniende kasi kuliko kawaida.

Lilikuwa ni tukio ambalo almanusra liukatishe uhai wangu baada ya kuvamiwa na watu nisiowafahamu kwenye foleni, maeneo ya Magomeni Mataa ambao walinishambulia vikali na kunijeruhi vibaya na kitu chenye ncha kali kifuani.

“Ni yeye! Ni mwenyewe…” nilijikuta nikitamka kwa nguvu, Shamila na yule dereva teksi wakabaki kunishangaa, wakiwa hawaelewi nilichokuwa namaanisha.

“Upo sawa kweli? Kama kuna tatizo si uniambie mpenzi?” alisema Shamila huku na yeye akiwa makini kutazama kule nilikokuwa naangalia, ghafla nikamuona amekazia macho pale kwenye lile gari, naye akawa ni kama ameona kitu.

Kwa bahati nzuri, ile teksi tuliyopanda ilikuwa pia na vioo vyenye tinted kwa hiyo haikuwa rahisi kwa watu waliokuwa nje kutuona. Tulitulia kwa dakika kadhaa, wote tukiwa tunawatazama wale vijana ambao walionekana kama wanajadiliana kitu huku macho yao yote yakiwa upande zilipokuwepo wodi, hasa ile niliyokuwa nimelazwa mimi.

“Unawafahamu?”

“Ndiyo, wana ukaribu na Shenaiza na ndiyo waliohusika kwenye jaribio la kutaka kuyakatisha maisha yangu.”

 

“Sasa hapa watakuwa wamefuata nini?”

“Kuna mawili, wanaweza kuwa wamemfuata Shenaiza au wamenifuata mimi.”

“Wakufuate wewe? Kwa kipi hasa?”

“Nimeshakwambia kuwa ni hawa ndiyo walioshiriki kwenye jaribio la kutaka kuyakatisha maisha yangu, yule mmoja namkumbuka vizuri kabisa.”

“Basi kama ni hivyo kwa nini tusiwapigie simu walinzi wa hospitali wawasiliane na polisi na kuwakamata? Mimi nina namba za mlinzi wetu wa kule getini,” alisema Shamila huku akitoa simu yake lakini nikamzuia.

Yule dereva teksi aliendelea kutulia kama haelewi chochote kinachoendelea, tukaendelea kujadiliana mle ndani ya teksi kwa muda mrefu huku nikiwa nimekosa kabisa amani.

Hakuna kitu kibaya maishani kama kuwaona wabaya wako lakini ukawa huna namna ya kulipa kisasi, nikaamua kufuata ule usemi maarufu ambao Waingereza hupenda kuutumia; ‘dont hunt what you can’t kill’ wakimaanisha usiwinde usichoweza kukiua!

Tukiwa bado tumetulia pale kwenye gari, ghafla kwa mbali tulimuona mtu aliyekuwa amevalia mavazi ya kidaktari akitoka kwenye wodi niliyokuwa nimelazwa, akatazama huku na kule kama anayetafuta kitu kisha akatembea harakaharaka mpaka pale kwenye lile gari, akawa anazungumza na wale watu waliokuwa mle ndani ya lile gari huku mara kwa mara wakigeuka kutazama kama kuna mtu aliyekuwa akiwatazama.

“Mungu wangu, nini kinachoendelea hapa? Mbona huyu aliyevaa kama daktari siyo mfanyakazi hapa hospitalini?”

“Siyo daktari? Kivipi? Na kama siyo daktari mbona amevaa nguo za kidaktari na ameingia hadi wodini?”

“Niamini ninachokwambia, madaktari wote wa hapa nawafahamu, huyu siyo mfanyakazi,” alisema Shamila kwa kujiamini, nikaiona hatari kubwa iliyokuwa mbele yangu. Kwa tafsiri nyepesi, mtu huyo alikuwa akishirikiana na wale watu waliokuwa ndani ya gari.

Kilichozidi kunishangaza, aliwezaje kuingia mpaka ndani ya wodi niliyokuwa nimelazwa bila kugunduliwa na walinzi wa hospitali hiyo? Kama angekuwa na nia ya kunidhuru ingekuwaje?” nilijikuta kijasho chembamba kikinitoka.

Waliendelea kujadiliana pale kwenye gari kisha tukamuona yule aliyejifanya daktari akivua koti lake jeupe na kuliweka kwenye siti za nyuma za gari, akaingia kwenye gari, milango ikafungwa na gari hilo ambalo muda wote lilikuwa likinguruma taratibu bila kuzimwa (silencer), likaanza kurudi nyuma likitafuta upenyo wa kutoka kwenye maegesho hayo.

Muda mfupi baadaye, liliondoka kwa kasi kubwa huku likitimua vumbi bila kujali kwamba eneo hilo lilikuwa ni hospitali na kulikuwa na wagonjwa waliokuwa wakihitaji utulivu, nikashusha pumzi ndefu na kuegamia kwenye siti niliyokuwa nimekaa, Shamila naye akafanya hivyohivyo.

“Sasa itakuwaje?”

“Sipo tayari kuendelea kulazwa kwenye hii hospitali, ni bora nikafie mbele ya safari, hapa si sehemu salama tena,” nilimjibu Shamila, akawa anatingisha kichwa kuonesha kuniunga mkono kwa kile nilichokuwa nakisema.

Tukiwa bado ndani ya teksi ile, nilishtuka sana baada ya kumuona Raya akifungua mlango na kutoka kwenye ile wodi niliyokuwa nimelazwa, mkononi akiwa amebeba kikapu kilichokuwa na chakula, akionesha kuwa na huzuni kubwa ndani ya moyo wake.

Baada ya kutoka wodini, alikaa kwenye benchi lililokuwa pale nje na kuweka kikapu chake chini, akawa anatazama huku na kule huku akionesha kuwa na wasiwasi mkubwa ndani ya moyo wake. Kwa kumtazama tu, japo nilikuwa kwa mbali, nilielewa kilichokuwa kikipita ndani ya kichwa chake, nikajikuta nikimuonea huruma sana.

Kumbe wakati nikimtazama Raya kwa huruma, Shamila naye alikuwa akinitazama usoni! Haya mambo ya mapenzi hatari sana, akashikwa na wivu mkali, akanizindua kwa kunigeuza kule nilikokuwa natazama na kunigeuzia kwake.

>>>Usikose kutembelea Simulizi za Majonzi

“Uko sawa?” aliniuliza huku hisia kali za wivu zikijionesha waziwazi kwenye uso wake.

“Nitakuwaje sawa katika mazingira kama haya? Naomba unisaidie jambo, kamuulize Raya yule daktari feki alipoingia wodini amesemaje?” nilimwambia Shamila, akaendelea kunitazama machoni huku akionesha dhahiri kwamba kuna jambo alikuwa anataka kuniambia.

Kwa shingo upande alishuka na kutuacha mimi na dereva teksi ndani ya ile teksi, aliposhuka tu, nilimwambia dereva aloki milango, tukawa tunamtazama Shamila anavyotembea kwa maringo kuelekea kule nje ya wodi alikokuwa amekaa Raya.

“Vipi kaka ndiyo unakaa hapa nini?” aliniuliza yule dereva teksi kwa lugha za vijana, akimaanisha kama mimi ndiye niliyekuwa nikitoka kimapenzi na Shamila, nikashindwa cha kumjibu kwani kwa muda huo akili yangu ilikuwa ikienda ‘resi’ sana, akaendelea:

“Duh! Si mchezo, utakuwa unafaidi sana, bonge la kifaa, ningekuwa mimi ningetangaza ndoa kabisa!”

Alikuwa na haki ya kusema hivyo kwa sababu kama nilivyoeleza awali, Shamila alikuwa mwanamke aliyejaaliwa uzuri wa kipekee mno, ukichanganya na umbile lake lililojazia kwa nyuma, hakuna mwanaume ambaye amekamilika angeweza kupishana naye bila kugeuka mara mbilimbili.

Japokuwa alikuwa amevaa nguo zake za kazini, uzuri wake haukuweza kujificha, nikajikuta kwenye wakati mgumu kwani Raya nilikuwa nampenda na alikuwa na mapenzi ya dhati kwangu, ukichanganya pia kwamba mimi ndiye niliyekuwa mwanaume wake wa kwanza maishani, nilijihisi kuwa sehemu ya maisha yake!

Niliendelea kutulia mle ndani ya teksi, Shamila akaenda mpaka pale Raya alipokuwa amekaa huku amejiinamia, alipomuona Shamila tu, harakaharaka alisimama na kumsogelea, akawa anamuuliza jambo ambalo japokuwa sikuwa nasikia, nilitambua kwamba ananiulizia mahali nilipokuwa mimi ‘mgonjwa wake’.

Tofauti kabisa na tulivyokubaliana, nilishangaa Shamila akimuonesha kwa kidole kwenye ile teksi niliyokuwemo, nikamuona Raya akiacha kila kitu palepale na kuanza kutimua mbio kuja kwenye ile teksi, Shamila akawa amesimama akimtazama. Nilijua wazi kwamba amefanya hivyo kwa sababu ya wivu.

Ghafla akiwa anakuja mbio, lile gari lilitokeza tena na kuja kwa kasi pale lilipokuwa limepaki awali, nikashtuka kugundua kuwa kumbe wale watu hawakuwa wameondoka, nikajua lazima watashtukia mahali nilipo kutokana na jinsi Raya alivyokuwa anakuja kwa kasi.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue au bofya Simulizi za Majonzi.

Leave A Reply