The House of Favourite Newspapers

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 5

0

ILIPOSHIA:

Aliniambia Shenaiza amerejewa na fahamu na jambo la kwanza alilouliza ni kama nilikuwa nimempigia simu.

“Nimemwambia kwamba upo hapa nje, akaniomba sana akuone, lakini anazungumza kwa shida sana,” alisema nesi huyo, nikainuka na kuanza kumfuata harakaharaka kuelekea wodini.

SASA ENDELEA…

Muda mfupi baadaye, tulikuwa pembeni ya kitanda alichokuwa amelazwa msichana huyo, nesi Rozina akaniambia ananipa dakika chache za kuzungumza na mgonjwa, akatoka na kufunga mlango wa wodi hiyo. Kwa muda wote huo, macho yangu yalikuwa juu ya uso wa msichana huyo ambaye naye alikuwa akinitazama, tukawa tunatazamana.

Tofauti na nilivyofika mara ya kwanza hospitalini hapo, safari hii niliweza kumuona vizuri msichana huyo. Kitu ambacho naomba nikiseme wazi, japokuwa alikuwa kwenye maumivu makali, akiwa amefungwa bandeji kubwa kichwani na jicho lake moja likiwa limevilia damu na kuwa jekundu, Shenaiza alikuwa na sura nzuri mno.

Nilijikuta nikivutiwa naye na kuendelea kumtazama, naye akawa ananitazama bila kusema kitu chochote mpaka nilipoamua kuvunja ukimya.

“Pole dada Shenaiza! Pole sana,” nilisema kwa sauti ya upole, kauli yangu ikawa kama mkuki ndani ya moyo wake kwani badala ya kujibu, alianza kuangua kilio kikali cha kwikwi, machozi mengi yakawa yanachirizika kupitia kwenye pembe za macho yake na kuishia kwenye shuka jeupe alilokuwa amelala juu yake.

Ikabidi nimsogelee zaidi na kumuinamia pale kitandani, kwa kutumia mkono wangu mmoja nikawa namfuta machozi huku nikiendelea kumpa maneno ya kumfariji, nikamuona naye akitoa mkono wake mmoja kwenye shuka na kuushika mkono wangu huku akiendelea kulia, akauvutia kifuani kwake huku akinitazama usoni.

Macho yake ni kama yalikuwa na sumaku kwani katika mazingira ambayo sikuyategemea, na mimi nilijikuta nikianza kulengwalengwa na machozi. Nilijikuta nikimuonea mno huruma msichana huyo na kuwa na shauku kubwa ya kutaka kusikia nini kilichomtokea.

Mpaka muda huo, hakuwa amefumbua mdomo wake na kuzungumza neno hata moja zaidi ya kuendelea kulia tu huku akinitazama kwa macho yaliyobeba ujumbe. Japokuwa na mimi nilijisikia uchungu sana, nilijitahidi kujikaza kiume na kuendelea kumbembeleza.

“Nashukuru kwa upendo wako ulionionesha, kumbe nilivyokuwa nimekutafsiri baada ya kusikia sauti yako mara ya kwanza nilipokosea namba yako ya simu nilikuwa sahihi kabisa,” alisema Shenaiza kwa sauti ya chini mno lakini iliyosikika vizuri kabisa masikioni mwangu.

“Usijali Shenaiza, nipo kwa ajili yako na nitaendelea kuwepo pembeni yako kwa shida na raha,” nilimwambia, kauli ambayo ilimfanya aachie tabasamu hafifu, akaubusu mkono wangu ambao muda wote alikuwa bado ameung’ang’ania.

Kilichonishangaza kwa Shenaiza, japokuwa ndiyo kwanza tulikuwa tunakutana kwa mara ya kwanza, tena akiwa kwenye maumivu makali, alionesha kama ana hisia fulani juu yangu kwa sababu siyo rahisi kumshika mkono kisha ukaubusu kwa mtu ambaye wala hujawahi kumuwazia akilini mwako.

“Halafu kumbe wewe ni kijana mzuri namna hiyo, kwa nini hujaoa mpaka leo,” alisema Shenaiza kwa lafudhi nzuri japo alionesha kuwa na maumivu, nikajikuta nikitabasamu na kukosa cha kumjibu.

“Kwani nini kimekutokea dada’angu?”

“Ni stori ndefu, ngoja nitakusimulia kila kitu nikipata nafuu lakini naomba umwambie na nesi kwamba sihitaji mtu yeyote ajue kwamba nimelazwa hapa, naweza kupata matatizo mengine bure. Naomba wewe ndiyo uwe mtu pekee wa kunisimamia mpaka nitakapopona,” alisema msichana huyo kwa sauti ya chini iliyoonesha bado yupo kwenye maumivu, nikawa natingisha kichwa kuonesha kukubaliana naye.

Kwa muda mfupi niliozungumza na Shenaiza, niligundua kwamba huenda ana jambo zito sana lililokuwa likiusumbua moyo wake na kweli alikuwa akihitaji mtu wa kumsaidia ingawa bado sikuwa najua ni nini kilichokuwa kinamsumbua.

“Nikuulize swali jingine?” nilimhoji, akatingisha kichwa kuonesha kukubali. Nilitaka kumuuliza kuhusu jinsi alivyokuwa amenisevu kwenye simu yake lakini nikahisi huenda nikam-boa kwa swali hilo.

“Uliza tu,” alinisisitiza baada ya kuona nasitasita.

“Kwa nini umenisevu vile kwenye simu yako?”

“Simu yangu? Mungu wangu, we umeonaje wakati hata simu yangu huijui,” alisema msichana huyo huku aibu za kikekike zikiwa zimetawala kwenye uso wake, akawa anakwepesha macho yake ili yasigongane na yangu, tabasamu hafifu likiwa limechanua kwenye uso wake.

Aliendelea kulikwepakwepa swali hilo lakini na mimi niliendelea kumbana hapohapo. Nilichokifanya, niliamua kuipiga namba yake na kwa kuwa simu yake ilikuwa pembeni ya kitanda chake ingawa mwenyewe hakuiona, muda mfupi baadaye ilianza kuita, namba yangu ikiwa imeseviwa ‘My Husband’! Akazidi kujisikia aibu za kikekike na mwisho akafunguka:

“Niliamua kukusevu hivyo kwa sababu ya matatizo yanayonikabili, naomba suala hilo tusilizungumze leo, ipo siku utanielewa,” alisema na kugeukia pembeni kuonesha hakuwa akitaka tuendelee kuzungumzia suala hilo, nikabadilisha mada haraka.

Kingine kilichonishangaza kwa Shenaiza, kila nilichokuwa namuuliza alikuwa akikwepa kunijibu, hakuna jambo hata moja ambalo nilitaka kulijua na akanijibu bila wasiwasi, nilipomuuliza anaishi wapi na anakaa na nani, alikwepa swali hilo kwa maelezo kwamba tutazungumza siku nyingine akiwa amepona.

Nilipomuuliza pia nini kilichomtokea mpaka akaumia hivyo mpaka kulazwa hospitalini hapo, bado hakuwa tayari kunieleza, kisingizio kikawa kilekile kwamba mpaka atakapopona ndiyo atanieleza kila kitu.

Kwa kuwa bado mwili wake haukuwa na nguvu hasa baada ya kupoteza damu nyingi kama alivyonieleza nesi Rozina, nilikubaliana naye. Nilipomuuliza kama angehitaji nini usiku huo kwa ajili ya chakula kwa sababu nilikuwa na uhakika kwamba hajala chochote, aliiambia nikamtafutie juisi tu, inamtosha.

Tayari nesi alishaingia na kunitaka nitoke kwani mgonjwa alikuwa akihitaji mapumziko ya kutosha, nikamwambia kwamba kuna vitu ameniagiza naenda kumnunulia nitarejea baada ya muda mfupi, nesi akaniruhusu huku akisisitiza niwahi kwani kuna muda ukishafika, watu wa kawaida hawaruhusiwi tena kuingia wodini.

Nilitoka haraka na kwenda kwenye maduka yaliyokuwa jirani na hospitali hiyo, nikamnunulia juisi maboksi mawili na keki laini ambazo niliamini atazipenda. Nikarudi wodini na muda mfupi baadaye niliruhusiwa tena kuingia wodini, nikamkuta Shenaiza ametulia pale kitandani, akionesha kuanza kupata ahueni kubwa. Aliponiona tu, tabasamu pana lilichanua kwenye uso wake, nikamsogelea mpaka pale kitandani, nikatoa maboksi ya juisi na keki na kuweka kwenye droo ya pembeni ya kitanda na kumtaka akijisikia ahueni ajitahidi kunywa.

Kwa kuwa muda nao ulikuwa umeyoyoma, nilimuaga kwamba narudi nyumbani lakini nitakuja kumtembelea asubuhi lakini alionesha kuwa mgumu kukubaliana na hilo.

Mara simu yake ilianza kuita mfululizo, akaishika na kutazama namba ya mpigaji lakini katika hali ambayo sikuielewa, aliiachia simu hiyo, ikadondoka chini na kufunguka betri ikaangukia kivyake, mfuniko kivyake na simu nayo kivyake. Akaanza kuangua kilio kwa uchungu huku akiniomba nimsaidie, nilibaki nimepigwa na butwaa.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue au bofya Simulizi za Majonzi

Na Hashim Aziz: 0719401968.

Leave A Reply