The House of Favourite Newspapers

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 51

ILIPOISHIA:

“Sikuwahi kudhani kwamba unaweza kuwa na nguvu kubwa kiasi hicho, hongera sana, utanifaa sana wewe,” alisema huku akipitisha mkono wake mmoja begani kwangu kichovu kisha akanigeukia, tukawa tunatazamana. Katika hali ambayo sikuitegemea hata kidogo, nilishangaa yule mwanamke akinibusu, tena mdomoni, nikashtuka mno.

“Hongera sana, ila inabidi upunguze mambo ya wanawake, utakuwa na nguvu zaidi ya hizi ulizonazo,” aliniambia huku akinitazama usoni.

SASA ENDELEA…

“Sijakuelewa,” nilimwambia, akashusha pumzi ndefu na kukaa vizuri pale juu ya zulia. Bado si Raya, Shamila wala Firyaal waliokuwa wamezinduka.

“Utanielewa tu,” inabidi kwanza tukaoge kuondoa uchovu halafu tuwasaidie na hawa nao warudi kwenye hali yao ya kawaida, tuna kazi nyingine ya kumsaidia Shenaiza, ni lazima arudiwe na fahamu zake, tena ikiwezekana haraka iwezekanavyo,” alisema mwanamke huyo kisha akapiga miayo mfululizo na kujinyoosha.

“Kwa kawaida, kila binadamu huwa anazalisha nguvu, nadhani hilo nilishakueleza kutoka mwanzo ingawa ni wachache sana wanaolitambua hili.

“Yaani ni kama kupepesa kope, unajua ni mpaka mtu akukumbushe kwamba muda wote macho yako yanapepesa kope ndiyo unakumbuka?” alisema, nikawa sioni chochote kipya kwenye mazungumzo yake kwa sababu ni jambo ambalo nilikuwa nimeshalisikia sana maishani mwangu kwamba kila binadamu anazalisha nguvu zisizoonekana.

“Nguvu tunazozalisha huwa zinatengeneza kitu kinachoitwa aura ambacho wengine huwa wanakiita ni mwili usioonekana juu ya mwili unaoonekana. Sasa kwa mtu mwenye utambuzi wa nguvu hizi, anao uwezo wa kuuona mwili huu.

“Kwa mtu ambaye anaishi maisha ya kitakatifu, yaani hanywi pombe, havuti sigara, hafanyi zinaa, hawasemi vibaya watu wengine, hana wivu wala kinyongo, ana upendo wa dhati kwa watu wote na ambaye moyo wake uko safi, hii aura huwa na kawaida ya kung’aa sana. Mtu akikutazama tu anaiona nguvu inayokuzunguka.

“Lakini vilevile kama mtu anaishi maisha ya hovyo, pengine ni mlevi sana, anafanya ngono hovyohovyo, ana wivu, hasira, vinyongo na tabia mbayambaya, kwa kawaida huwa aura yake inafifia sana na kama una utambuzi wa nguvu hizi, ukimtazama tu unamjua ndiyo maana nilikwambia vile,” alisema yule mwanamke na kuzidi kunishangaza.

Kitu alichokisema sikuwa nimewahi kukisikia sehemu yoyote, nikabaki nimepigwa na butwaa, akaendelea:

“Japokuwa watu wengi huwa hawaelewi kuhusu aura kwa hiyo hawajui umuhimu wa kuishi kitakatifu hata kama huna dini, siyo kitu cha mchezomchezo. Aura ya mtu huanza kuishi kabla mtu hajazaliwa na huendelea pia mpaka mtu anapokufa. Ndiyo maana mtoto anapokaribia kuzaliwa, tafiti zinaonesha kwamba huwa ana uwezo wa kuelewa kinachoendelea kwenye ulimwengu wa nje.

“Hii ni kwa sababu tayari mwili wake ambao hauonekani unakuwa umeshaingia kwenye ulimwengu wa kawaida. Akishazaliwa, huwa inatakiwa mwili wake halisi uungane na hii aura na hiyo hufanyika katika kipindi cha siku arobaini tangu mtoto azaliwe ndiyo maana kuna tamaduni nyingi kwamba mtoto anatakiwa kuanza kutolewa nje baada ya siku arobaini kwani pale inakuwa tayari aura yake na mwili halisi vinakuwa vimeungana hivyo anakuwa na kinga dhidi ya mambo mabaya yasiyoonekana kwenye ulimwengu wa kaiwada.

“Hiyo pia hutokea pale mtu anapokufa ambapo nafsi inapotengana na mwili, aura huwa inaendelea kuishi mpaka baada ya siku arobaini ndiyo nayo hutoweka, ndiyo maana pia huwa kuna tamaduni za kufanya arobaini ya marehemu kwani pale ndiyo uhai huwa unakuwa umefikia mwisho.”

Maelezo hayo yalinifanya nikune kichwa kwani siyo siri yalikuwa yamenichanganya sana akili. Ni mambo ambayo sikuwahi kuyasikia kabla lakini kwa jinsi alivyokuwa akiyafafanua, ilionesha dhahiri kwamba ni kweli. Hata mimi sikuwahi kupata jibu la kwa nini mtoto anatakiwa atolewe nje baada ya siku arobaini tangu azaliwe na kwa nini mtu akifa, msiba huwa unahitimishwa baada ya siku arobaini.

“Lakini mamdogo…”

“Usiniite mamdogo, ningependa zaidi uniite kwa jina langu halisi ambalo ni watu wachache huwa wanalijua. Nina majina mengi lakini jina langu halisi ni Junaitha,” alisema huku akiinuka pale alipokuwa amekaa.

“Hakuna cha lakini… punguza wanawake ili aura yako ing’ae na kukuongezea nguvu, mimi sijui nina mwaka wa ngapi simjui mwanaume,” alisema huku tayari akiwa amesimama, akanipa mkono kama ishara ya kutaka anisaidie kuinuka.

Nilibaki kumtazama tu usoni, mambo mengi yalikuwa yakipita ndani ya kichwa changu.

“Mbona unanitumbulia macho? Amka twende ukaoge, bado kuna kazi kubwa leo,” alisema yule mwanamke, nikampa mkono, akanishika na kunivuta kidogo, nikasimama.

“Halafu inatakiwa pia uwe makini na vyakula unavyokula, inaonesha mwili wako hauna uzito unaotakiwa, hata hao wanawake unaotembea nao hovyo huwa unawaridhisha kweli? Wanaume wa siku hizi wana tatizo kubwa la upungufu wa nguvu za kiume, na wewe usije kuwa miongoni mwao,” alisema huku akitabasamu.

Japokuwa mwenyewe alichukulia kama masihara lakini kwa hulka za kiume, niliona kama amenidharau sana. Maneno yake ni kama yalikuwa yakihitaji nifanye kitu fulani kumthibitishia kwamba sikuwa mtu wa mchezomchezo bali mwanaume niliyekamilika.

Nilipounganisha na tukio la yeye kunibusu kwenye midomo yangu wakati akinipongeza, akili nyingine zilianza kupita ndani ya kichwa changu.

“Kwa hiyo unaishije bila mume?”

“Kwani wewe unapata faida gani kubadilishabadilisha wanawake?” aliniuliza swali juu ya swali ambalo lilinifanya nijiulize sana kwa nini alikuwa akinikomalia kuhusu suala la mimi kuwa na wanawake wengi. Elimu aliyonipa ilikuwa imetosha kunifanya nijitambue lakini kwa nini alikuwa akiendelea kuulizauliza kuhusu mimi kuwa na wanawake? Sikupata majibu.

“Mbona unakuwa mkali sana kwangu Junaitha? Au kuna kitu nimekuudhi?”

“Ndiyo umeniudhi, kwa nini kijana mtanashati kama wewe usitafute mwanamke mmoja tu anayejitambua ukatulia naye?” nilijikuta nikishindwa kujizuia, nikaangua kicheko kwani tayari nilishaanza kupata picha ya kilichokuwa kikiendelea ndani ya kichwa chake.

“Kwa hiyo unanidharau si ndiyo? Yaani mi naongea mambo ya maana wewe unacheka,” alisema, akatoka na kuniacha nimesimama palepale, nikiwaangalia wale waliokuwa wamelala juu ya zulia, kila mmoja akiwa hajitambui kwa uchovu.

“Hebu njoo huku,” nilisikia sauti ya Junaitha ikitokea chumbani kwake, harakaharaka nikatoka pale na kuelekea kule sauti ilikokuwa inatokea.

“Ingia tu mlango upo wazi,” alisema, nikageuka huku na kule kwanza kwa sababu sikuona kama ni heshima kwa mtoto wa kiume kuingia chumbani kwake, hasa ukizingatia ukweli kwamba alikuwa amenizidi sana umri. Nikapiga moyo konde na kuingia ndani ya chumba hicho cha kisasa kilichokuwa na vitu vingi vya thamani.

“Chukua taulo pale kabatini ingia bafuni ukaoge,” alisema akiwa amekaa juu ya kitanda kikubwa cha kisasa akihangaika kufungua zipu ya gauni alilokuwa amevaa, nikaelekea pale kwenye kabati aliponielekeza, nikachukua taulo na kuanza kuelekea kwenye lile bafu la ndani kwa ndani kule chumbani kwake.

Nililazimika kuingia na nguo zote bafuni kwani nilikuwa naona aibu kuvua hata shati mbele ya macho yake.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue au bofya Simulizi za Majonzi kusoma mwendelezo.

Comments are closed.