The House of Favourite Newspapers

SEVEN DAYS IN HELL (SIKU SABA KUZIMU)- 57

ILIPOISHIA:

“Jamal! Jamal! Amka, kuna tatizo,” sauti ya Junaitha ndiyo iliyonizindua kutoka kwenye usingizi fofofo, nikakurupuka nikiwa na shauku kubwa ya kutaka kujua kumetokea nini tena.

SASA ENDELEA…

“Kuna nini tena?”

“Huyu mshenzi anataka kunizidi nguvu, amka ukanisaidie,” alisema Junaitha, huku kijasho chembamba kikimtoka. Harakaharaka nikakurupuka na kuvaa bukta na fulana, nikaongozana na Junaitha ambaye tayari alishatoka na kuanza kukimbilia kule kwenye chumba chake cha siri.

Tulipokaribia nilisikia sauti za kutisha mno, yule mwanamke tuliyemteka akawa ananguruma kama mnyama wa porini huku akikwangua mlango wa chuma kwa kucha zake ngumu, akitaka kutoka.

“Nisikilize! Jamal nisikilize,” alisema Junaitha ambaye alikwama ghafla pale mlangoni.

“Tukifungua mlango atatuzidi, inabidi tuingie kwa kutumia nguvu zetu tukapambane naye hukohuko ndani, amenitia meno, si unaona,” alisema Junaitha huku akinionesha alama ya meno mkononi mwake, huku damu nyeusi zikichuruzika.

Kumbe zile kelele ziliwashtua Raya, Firyaal na Shamila ambao kwa muda mrefu walikuwa wamelala fofofo kutokana na uchovu, nao wakawa wanakuja kwa kujikokota, kila mmoja akionesha kuwa na hofu kubwa ndani ya moyo wake.

“Msije, nyie ishieni hapohapo,” alisema Junaitha kwa sauti ya juu, wote wakafunga breki na kuanza kututazama.

“Inabidi tupeane migongo na kuunganisha mikono ili tuingie kwa urahisi, haya sogea,” alisema. Bila kupoteza muda nilifanya kama alivyoniambia, tukashikana mikono kwa nguvu, mkono wake wa kulia ukaushika wangu wa kushoto na wangu ukamshika yeye kwa namna ya kubadilishana, kushoto na kulia.

Alinielekeza tufumbe macho, tulipofumbua tayari tulikuwa ndani ya chumba hicho cha siri ambacho sikuwahi kuingia hata siku moja, yule mwanamke akawa anaendelea kusumbua pale mlangoni bila kujua kwamba tayari tulikuwa nyuma yake.

“Kumbe ana kamba nyingine pale shingoni, inabidi ufanye kama tulivyofanya kule porini, kaikate kwa nguvu, usijali hata akikuumiza dawa ipo, ishinde hofu,” alisema Junaitha, nikawa namsogelea kwa kunyata, mara nikakanyaga kitu chini kilichofanya niteleze na akuanguka kama mzigo, puuh!

Kishindo cha kuanguka kwangu kilimshtua yule mwanamke ambaye sasa macho yake yalikuwa yamebadilika na kuwa ya kung’aa kama mnyama mkali wa porini anavyong’aa gizani.

Nilipotupia macho haraka kwenye kitu kilichofanya niteleze, nilishtuka mno baada ya kugundua kuwa ilikuwa ni mifupa ya fuvu la mtoto mdogo.

“Ishinde hofu, kamilisha kazi kwanza mengine baadaye,” alisema Junaitha, nilipogeuka kumtazama yule mwanamke, bado alikuwa amenikazia macho huku akiendelea kunitazama kwa ukali, udenda mwingi ukitoka na meno yake makali yakionekana.

Kwa ujasiri wa hali ya juu nilisimama, yule mwanamke naye akakaa mkao wa kutaka kushambuliana na mimi, tukawa tunatazamana. Kiukweli alikuwa akitisha sana lakini sauti ile ilisikika tena ndani ya moyo wangu kwamba natakiwa kuishinda hofu.

Kwa kasi ya ajabu nilimrukia yule mwanamke, kutokana na uzito wangu nikamzidi nguvu na kudondoka naye mpaka chini, akapiga kelele kwa nguvu zaidi kisha akanikamata mkono wa kushoto na kuning’ata kwa nguvu.

Kwa jinsi meno yake yalivyokuwa makali, nilihisi kama mkono wangu unakatika lakini nikapiga moyo konde na kumkamata shingoni, nikafanikiwa kukamata kamba nyingine ngumu na kuivuta kwa nguvu zangu zote, ikakatika na kumfanya yule mwanamke wa ajabu aishiwe nguvu, akadondoka kama mzigo na macho yake yakabadilika na kurudi kwenye hali ya kawaida.

“Unaniuaaa! Jamal unaniuaaa,” alisema huku akilitaja jina langu, nikashangaa sana amelifahamu vipi jina langu?” kabla sijajibu chochote, Junaitha alimrukia pale chini na kumkaba shingoni, akaanza kumzibua makofikwa hasira.

“Safari hii ukirudia tena nakuchinja kwa mikono yangu,” alisema Junaitha, tukasaidiana kumfunga tena kamba na safari hii, tulimfunga mikono kwa nyuma na kuunganisha na miguu, akawa analia kwa uchungu huku akisema tumsamehe kwani na yeye ana familia hivyo hayupo tayari kufa.

“Leo utasema kila kitu, wewe si unajifanya mshenzi,” alisema Junaitha na kabla ya yote, akamtaka kwanza mwanamke huyo amtibu jeraha alilomng’ata mkononi pamoja na lile alilokuwa amenijeruhi mimi kwenye mkono wangu wa kushoto.

Kama ilivyokuwa mwanzo, mwanamke huyo alitoa ulimi wake mrefu uliokuwa na mabakamabaka na kumlamba kwenye lile jereha, mvuke kama moshi ukatoka kisha taratibu likaanza kujifunga.

Na mimi nikasogea ambapo alifanya hivyohivyo lakini cha ajabu, mwanamke huyo alinitazama kwa namna ambayo sikuielewa, ni kama aliyekuwa anataka nitafute upenyo wa kuzungumza naye tukiwa wawili tu.

Kwa muda wote huo bado sikuwa nimepata nafasi ya kukichunguza vizuri kile chumba, ni mpaka jeraha langu lilipoanza kupunguza maumivu ndipo nilipopata akili ya kutaka kutazama vizuri kwanza lile fuvu lililosababisha nijikwae, kuteleza na kuanguka na vitu vingine vilivyokuwa ndani ya chumba hicho.

Cha ajabu, Junaitha aliniwahi na kuniziba macho, nikamsikia akitamka maneno fulani kisha kufumba na kufumbua, tukajikuta tumetoka nje ya chumba hicho kimazingara, tukaangukia palepale tulipokuwa tumekaa awali tukijadiliana namna ya kuingia.

“Vipi mbona sielewi?”

“Usiwe na haraka Jamal, naomba uniamini kwanza hayo mengine yote utayajua, tumalize kwanza kazi yetu,” alisema Junaitha kwa sauti ya chini, akiwa ni kama hataki akina Raya, Shamila na Firyaal ambao bado walikuwa wamesimama palepale, wasikie.

“Lakini…”

“Lakini nini Jamal? Unanipenda hunipendi?”

“Nakupenda.”

“Basi naomba unisikilize ninachokwambia,” alisema kwa sauti ya kunong’ona, nikawa sina ujanja. Nilimsikia yule mwanamke kule ndani ya chumba cha siri akiangua kicheko kwa sauti ya juu. Sikuelewa kwa nini amecheka kiasi hicho, nikabaki na viulizo vingi ndani ya kichwa changu.

Baada ya kukubaliana na Junaitha, niligeuka na kuanza kurudi kule sebuleni, akina Raya, Shamila na Firyaal wakatukimbilia kwa pamoja na kunikumbatia mimi na Junaitha.

“Mpo salama jamani?”

“Tupo salama wala msijali, niliwaambia hii kazi ni nzito sana, vipi yaani nyie ndiyo mnaamka saa hizi?” alisema Junaitha, nikawaona kila mmoja akikosa cha kujibu.

“Sasa muacheni Jamal akapumzike, nyie njooni huku kuna dawa niwape maana inatakiwa mrudiwe na nguvu zenu, bado kuna kazi kubwa, si mnaona purukushani iliyopo?”

“Yule kule aliyekuwa ananguruma kama mnyama ni nani?” Firyaal aliuliza swali, nikawaona wenzake wote wakitingisha vichwa, kuunga mkono swali hilo.

“Ni stori ndefu kidogo, ngoja nitawaeleza lakini njooni kwanza huku niwape dawa,” alisema.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue au bofya>>>Simulizi za Majonzi kusoma mwendelezo.

Comments are closed.