MGOMBEA Ubunge wa jimbo la Buchosa wilayani Sengerema mkoani Mwanza kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Eric Shigongo leo Ijumaa, Septemba 25, 2020, amezindua rasmi kampeni zake za uchaguzi katika Uwanja wa mpira Nyakarilo.
Katika uzinduzi huo Shigongo aliambatana na Mkewake Veneranda Ephraim, Mgombea Ubunge jimbo na Geita Vijijini, Kamati ya CCM Wilaya, ndugu Joseph Kasheku ‘Msukuma’, Mgombea Ubunge jimbo la Sengerema Tabasamu, pamoja na aliyewahi kuwa Mbunge wa Nyamagana na Waziri wa Mambo ya Ndani, Lawrence Marsha na viongozi waandamizi wa chama.
Akizungumza na wananchi waliojitokeza katika Uwanja wa Nyakarilo kumsikiliza, Shigongo amesema iwapo atachaguliwa kuwa mbunge wa Buchiosa, atahakikisha anainua kiwango cha elimu kwa wilaya ya Buchosa.
“Hali ya Elimu katika Wilaya ya Buchosa kiukweli hairidhishi, kila matokeo ya kidato cha nne na sita yakitoka naangalia lakini kiukweli bado hali ya kielimu iko chini sana, endapo mkinichagua, nitahakikisha napambana ili Elimu katika wilaya yetu iwe juu na tuweze kushika nafasi za juu kitaifa katika matokeo ya jumla,” amesema Shigongo.
Aidha, Shigongo amesema licha ya kuwa na jukumu zito la kuhakikisha Jimbo la Buchosa linapata maendeleo ipasavyo atashirikiana na wavuvi katika wilaya hiyo kuona wanafanya kazi zao bila bugudha.
“Siku za hivi karibuni kumekuwa na tabia ya dhuruma kwa wavuvi hivyo nitahakikisha wavuvi wetu wanafanya kazi yao vizuri bila bughudha kwa kua na wao ni wananchi wenzetu, wanahitahi kufanya kazi kwa amami ili wakuze vipato vyao na kufurahia manufaa ya rasilimali za taifa lao,” amesema Shigongo.
Mgombea ubunge Jimbo la Geita Vijijini (CCM), Joseph Msukuma amesema; “Nawaomba wana Buchosa mumchague Shigongo kwa kua ni kijana ambaye amejitoa kwa dhati kuja kuwatumikia, namimi naomba nikuahidi Shingongo kwamba nitajitoa kuhakikisha unashinda uchaguzi ndiyo maana hata kabla Kampeni hazijaanza tulimwomba Rais Magufuli apite hapa kwa kua huku anakupenda sana hivyo lazima tuhakikishe CCM inashinda katika uchaguzi huu mkuu.
Uzinduzi wa Kampeni umenogeshwa na wasanii mbalimbali wakiwemo Young Killer, Joel Lwaga, H. Baba, Kundi la Komedi la Futuhi na wengine wengi ambao kila mmoja alifanya kazi yake ya kuhakikisha burudani katika Uwanja wa Nyakarilo inakwenda kama ilivyopangwa.
Habari/Picha na Johnson James- GPL BUCHOSA.