The House of Favourite Newspapers

Shehe Amuonya Sanchi Kubadili Dini

0

BAADA ya mwanamitindo mwenye umbo matata Bongo, Jane Rimoy ‘Sanchi’ kubadili dini na kuwa Muislam ambapo kwa sasa anajulikana kwa jina la Surraiya, Sheikh Ahmed Kandauma ameibuka na kumuonya, Risasi Mchanganyiko linakupa habari kamili.

 

Akizungumza na Risasi Mchanganyiko, shehe huyo alisema Sanchi kwa sasa anatakiwa kubadilika hasa kimuonekano, kwani awali kabla ya kubadili dini, alikuwa akivaa mavazi ya kubana na kumuonesha mwili wake ulivyo.

 

Alisema dini ya Kiislam inataka heshima ya hali ya juu, kwani mambo ya kukaa nusu utupu na kujiachia kihasara ni kuidhalilisha dini, hivyo Sanchi anatakiwa kujilinda sana na mambo hayo kwa sasa kama kweli amekuwa Muislam afuate sheria na taratibu za dini.

 

“Kwa sasa tunaendelea kumwangalia Sanchi kwa jicho lingine kama kweli amekuwa Muislam safi ambaye atafuata sheria za dini na kuachana na mambo yale ya zamani ya kukaa nusu utupu au kuvaa nguo zinazobana na kumwonyesha alivyozaliwa.

 

“Kama kweli amebadili dini, basi anatakiwa kufuta hata yale mapicha ya kihasara aliyoweka kwenye ukurasa wake wa Instagram na aweke picha zenye stara ili kuonekana kweli ni Muislam safi,” alisema shehe huyo.

 

Kwa upande wa Sanchi, alisema ameamua kubadili dini kwa ridhaa yake mwenyewe na ni kitu ambacho alikipenda tangu zamani, hivyo kwa sasa amekamilisha ahadi yake aliyojiwekea.

 

“Nimebadilisha dini kwa kupenda mwenyewe, nilikuwa mdadisi sana wa dini ya Kiislam kutaka kuijua zaidi kwa sababu nilikuwa nafunga Ramadhan zilizopita, kwa hiyo nikajikuta nimeupenda sana Uislam,” alisema Sanchi.

 

Alipoulizwa kuhusu tetesi kwamba amebadili dini kwa sababu anataka kuolewa na Muislam, Sanchi alisema;

“Sijamfuata mtu wala hakuna ushawishi wowote, ni maamuzi yangu binafsi ambayo nimeona ni sahihi kwangu.”

 

Kuhusu wazazi wake kwamba wamelichukuliaje suala hilo, Sanchi alisema mama yake amefurahia sana licha ya kwamba ni Mkristo, hivyo hana shida.

Sanchi alieleza kuwa, amebadilika mpaka kimavazi, kwani ndiyo dhamira yake na anaamini Mungu atamuongoza kwenye hilo ili aweze kutimiza nguzo muhimu za Kiislam.

STORI | Imelda Mtema, Risasi

Leave A Reply