Shehe Ponda awaliza tena waislamu
Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Shehe Issa Ponda.
Na Makongoro OGING’
Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Shehe Issa Ponda aliyekuwa akituhumiwa kwa makosa ya uchochezi baada ya mahakama kutoridhishwa na ushahidi wa upande wa mashtaka na hivyo kuonekana hana hatia, kwa mara nyingine amewaliza tena Waislamu msikitini alipokuwa akiwasimulia waumini hao matatizo yaliyokuwa yakimwandama pamoja na kucheleweshewa haki yake kortini.
Akizungumza katika Msikiti wa Dini Moja Mungu Mmoja uliopo Morogoro wiki iliyopita baada ya kuachiwa huru na mahakama, Shehe Ponda alisema anawashukuru Waislamu wa Morogoro kwa jinsi walivyopigania maisha yake alipokuwa mikononi mwa polisi.
Shehe Khatwibu Yusufu Jumaa.
“Sisi ni viongozi kama viongozi wengine tena tunaongoza jamii, kulinda masilahi yao na kusimamia haki zao za msingi. Kwa hiyo ni lazima tuzisimamie na kuzilinda kwa haki na uandilifu,” alisema Shehe Ponda huku akiwashukuru akina mama waliokuwa wakifika mahakamani kusikiliza kesi yake.
Akizungumzia kuachiwa kwa Shehe Ponda, kiongozi wa Msikiti wa Masjid Haaqa, Buguruni, Shehe Khatwibu Yusufu Jumaa (pichani) aliyekuwa Morogoro alisema watakuwa bega kwa bega na kiongozi huyo kwani anafanya kazi za Mungu.
“Tupo pamoja na Shehe Ponda na nilikuwa naye Morogoro, tunaungana naye kuhakikisha jamii inatendewa haki. Binafsi nampongeza Rais John Magufuli kwa kasi aliyoanza nayo, anakwenda kulekule katika kutetea haki za wananchi,” alisema Shehe Khatwibu.
Shehe Ponda alifutiwa kesi yake ya uchochezi wiki iliyopita na kuachiwa huru na Hakimu Moyo wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro.