
MBUNGE wa Buchosa, Mhe. Eric Shigongo, amefunguka mbele ya Waziri wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Selemani Jafo, kuhusu adha wanayoipata wananchi wa jimbo hilo kutokana na ubovu wa barabara huku akimuomba kuiongezea fedha Mamlaka ya Barabara Vijijini (TARURA) ili waweze kutengeneza kwa haraka miundombinu ya barabara hizo katika kipindi hiki cha mvua nyingi zinazoendelea kunyesha jimboni humo na kuharibu barabara hizo mara kwa mara.
Shigongo amesema hayo jana Jumanne, Januari 5, 2021, wakati wa ziara ya kikazi ya Mhe. Jafo katika halmashauri ya Buchosa kukagua miradi mbalimbali inayotekelezwa na serikali ndani ya halmashauri hiyo.
Kwa upande wake Jafo amesema suala hilo amelichukua na ataenda kulifanyia kazi mara moja ili kurahisisha utendaji kazi wa TARURA katika Halmashairi ya Buchosa na waweze kutengeneza barabara ili wananchi wapitishe mazao yao na shughuli zao nyingine za kiuchumi.

