The House of Favourite Newspapers

SHILOLE HAKUSOMA, ALITELEKEZWA NA WATOTO; LEO NI STAA BONGO!

 

Zuwena Mohamed ‘Shilole’

ANAITWA Zuwena Mohamed ‘Shilole’, amezaliwa katika familia ya kimasikini huko Igunga, Tabora. Ni mtoto wa mwisho kati ya watoto watano, mama yake alifariki dunia miaka mingi iliyopita akiwa mtoto mdogo sana!

 

Wengi wanaweza kujiuliza, Shilole ni mwanamke wa chuma? Amefanya nini na amepitia nini kwenye maisha yake mpaka hapo alipofikia? Ukweli ni kwamba Shilole ni mwanamke wa chuma hasa. Mapito aliyopitia wangekuwa wengi wangekata tamaa na kutupilia mbali ndoto zao.

 

SIKIA KUHUSU SHULE

Shilole alisoma kwenye Shule ya Msingi Igunga na sekondari alinusa kwenye Shule ya Sekondari Igunda, ingawa hakumaliza baada ya kukatisha masono alipopata ujauzito.

 

ALIPATAJE UJAUZITO?

Akiwa na miaka kumi na nne, tena binti mdogo ambaye hajui mengi kuhusu dunia, Shilole amewahi kusimulia kuwa alifanyiwa kitendo cha kikatili kisha kupata ujauzito wa mtoto (jina tunalihifadhi) ambaye kwa sasa ana miaka 14.

 

Alipopata ujauzito huo, ingawa alikuwa anapenda sana shule ilimbidi akatishe masomo na alipojifungua aliendelea kukaa nyumbani kulea mtoto akifahamu maisha yake ndiyo yangekuwa hivyo na angeishia hukohuko kijijini.

Ili kuendesha maisha yake ilibidi aanze kuuza ndizi, maji na mikate stendi kwa wasafiri ambao walikuwa wanapita na mabasi ya mikoani. Baadaye akafungua genge sokoni huko kwao na kaunza kuuza vitunguu, nyanya na kabeji kisha akajitegemea kimaisha kwa kupanga chumba kwa shilingi 3,000 kwa mwezi!

 

AOLEWA NA DEREVA WA MAROLI

Maisha yaliendelea, baadaye Shilole akiwa na umri wa miaka 17 aliolewa na dereva wa magari makubwa ya mizigo aliyekuwa anamzidi miaka kumi, akaenda naye Dar, walifikia gesti huko Keko, kwa sababu aliyemuoa hakuwa na makazi na alimwambia waishi hapo ili atafute pesa za kupanga chumba. Baada ya mwezi, walipanga chumba huko Keko Brazil, baadaye akapata ujauzito wa mtoto wa pili na baadaye akajifungua.

 

MAISHA YA NDOA

Kuhusu maisha yake ya ndoa Shilole anasema kwamba yalikuwa na changamoto kubwa, mumewe hakuwa anamruhusu kufanya lolote lile, alimtaka kukaa tu ndani na alikuwa akimfanyia visa vingi.

Alidai alikuwa akimpiga kuliko kawaida kiasi kwamba mpaka sasa mguu wake wa kulia haupo sawa. Lakini baadaye mwaka 2009 kuelekea 2010, walishi-ndwana na ndoa ikavunjika na kupewa talaka. Hiyo ilikuwa ni miaka mitano baada ya ndoa na akaanza maisha mapya na watoto wake.

Kwa kuwa wakati wa ndoa alikuwa anajiiba na kusoma mambo ya hotelia, baadaye akapata kazi kwenye hoteli moja Kijitonyama.

RAY NDIYE ALIYEMTOA

Mbali na kwamba alikuwa na ndoto za kuwa mtu maarufu siku moja hasa kwa kuimba kwa maana alikuwa anampenda sana Ray C, lakini hakuwa na njia yoyote ambayo alikuwa anaiona ya kumfikisha kule alikokuwa anataka kwenda.

 

Lakini kama bahati siku moja, akiwa hotelini anafanya kazi alibahatika kukutana na Ray, aliyekwenda hotelini hapo. Akimhudumia alimweleza juu ya kependa kuigiza na Ray alimuachia namba ya simu. Akamtafuta na kumsumbua mpaka akakubali waonane. Ray akampa jaribio la kuigiza, akafanya na kuweza, kisha akapata nafasi ya kucheza kwenye muvi iitwayo Fair Decision, hapo ndipo safari yake ya kuwa staa ilipoanza.

JAMBO LA KUJIFUNZA

Kupitia Shilole hakika wewe uliyekata tamaa unaweza kujifunza mengi. Hebu jiulize, mtu ambaye hana elimu, mgeni jijini, mwanamke aliyeachika na mzigo wa watoto wawili kwa akili ya kawaida kuna namna angeweza kufikia ndoto zake kama si kwa kujiamini na kumtumainia Mungu?

 

Hakika isingewezekana. Lakini huyu Shilole ambaye hakuwa na elimu kama mastaa wengi, leo ni staa mkubwa Tanzania, anamiliki miradi kama vile mgahawa na kufanya shoo mbalimbali zinazomuingizia fedha, ana marafiki wengi ambao wanaweza kumsaidia kutimiza jambo lake lolote analopenda, hana njaa tena na pengine anaishi maisha ya ndoto zake hata kama baadhi ya ndoto hajazitimiza.

 

Kwa hiyo hii inatuonyesha kwamba inawezekana. Unaweza kuanzia hapo ulipo na kufika kule unakohitaji hata kama mazingira ni magumu mno!

Makala: Boniphace Ngumije.

Comments are closed.