Shoga; kwa nini UTI iwe kwako kila siku?
Asalaam alaykhum shoga yangu! Kwa upande wangu sijambo namshukuru Mwenyezi Mungu kwa hilo na nipo ofisini naandika mada ya wiki ijayo.
Shoga yangu, kwa kuwa safu hii ni mahususi kuandika mada zinazohusu mapenzi hasa namna ya kuyaboresha ili kukufanya wewe na mwenza wako kuyafurahia, leo nitazungumzia maradhi ya UTI ambayo yamekuwa yakileta usumbufu katika mapenzi.
UTI ambayo kirefu chake ni Urinary Tract Infection ikimaanisha kwamba ni maambukizi kwenye njia ya mkojo ni ugonjwa unaoambatana na mfumo mzima wa njia ya mkojo kutokea kwenye figo, mirija ya (ureter), kibofu, tunda (prostate gland) na njia ya kupitia mkojo kwenye uume (urethra).
Ugonjwa huu unaambukizwa kwa njia ya majimaji, choo kichafu, kujamiiana na mtu aliyeambukizwa UTI, pia kwa watu wanaopenda kufanya mapenzi kinyume na maumbile.
Kwa mujibu wa wataalam wa afya, UTI ni maradhi yanayowasumbua watu wengi hususan wanawake na watoto wadogo na ni ugonjwa ambao unasumbua sana na kuwafanya watu wakose raha.
Shoga yangu, kama kichwa cha mada hii kinavyojieleza hapo juu na chanzo cha maradhi hayo, ni wazi kama utakuwa mwangalifu siyo rahisi kuandamwa na UTI ambayo naweza kusema ni maradhi ya aibu.
Nasema ni maradhi ya aibu kwa sababu hayana tofauti kubwa na maradhi ya zinaa japo uambukizwaji wake hutokana na majimaji, vyoo vichafu na kufanya mapenzi na mtu mwenye UTI na wale watu wenye tabia ya kujamiiana kwa njia isiyo rasmi kama nilivyoeleza hapo.
Shoga; kama chanzo cha ugonjwa huo ni kutumia choo kichafu, kukutana faragha na mtu mwenye virusi vya UTI unashindwaje kujikinga kwa sababu ni mambo ambayo yapo ndani ya uwezo wako!
Nasema hivyo kwa sababu wapo baadhi ya wenzetu maradhi hayo yamekuwa sehemu ya maisha yao, jambo linalosababisha washindwe kushirikiana vyema na waume zao katika ‘mlo wa usiku’.
Kama umetulia na unahisi mwenza wako ndiye chanzo cha wewe kusumbuliwa na UTI mara kwa mara, kaa naye na mweleze athari za maradhi hayo ambayo yanaua kama maradhi mengine ili kuondokanayo kabisa kwa sababu nia aibu kwa mama kila kukicha kusumbuliwa na UTI. Zingatia masharti ya kuukwepa ugonjwa huo. Bye!