The House of Favourite Newspapers

Shule ya Mkapa Wakutwa Wakiiba Maji Usiku

SHULE ya Sekondari ya Anna Mkapa iliyopo kata ya Pasua katika Manispaa ya Moshi imebainika kufanya udanganyifu kwa kushiriki kitendo cha kuiba maji ya Mamlaka ya Majisafi na Mazingira mjini Moshi (MUWSA) kinyume cha sheria.

 

Mbali na wizi huo wa maji uliofanywa na wahusika kwa kuunganisha bomba katika maungio ya mita za maji, pia Mamlaka imebaini kupotea kwa mita ya kusoma kiwango cha maji kinachotumika iliyotolewa na MUWSA kwa shule hiyo ambayo ilipaswa kuwepo katika bomba hilo lililounganishwa kinyemela.

 

Tukio hilo lilibainika jana usiku majira ya saa 3:30 baada ya wafanyakazi wa MUWSA kufanya oparesheni ya kushtukiza katika shule baada ya kupokea taarifa kutoka kwa Wasamaria wema waliotoa taarifa kwa mamlaka juu ya wizi huo.

 

Akizungumza katika eneo la tukio, Ofisa Habari wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira mjini Moshi (MUWSA), Rashid Nachan, alisema kilichofanyika ni wizi na kwamba wahusika wanachangia kuhujumu uchumi wa nchi.

“Kinachoonekana hapa dhahiri ni kwamba uongozi wa shule unafahamu kinachoendelea kwa sababu hawezi kuja mtu kutoka nje kufanya kitendo cha kuondoa mita na kuweka bomba la moja kwa moja bila uongozi wa shule kufahamu.  Huyo atakuwa anafanya kwa faida ya nani sasa?” alihoji Nachan.

 

Alisema kinachoonekana, Shule ya Anna Mkapa imefanya kitendo hicho kwa muda mrefu na kwamba kimekuwa kikifanyika majira ya usiku na ikifika asubuhi hurudishia mita kama kawaida mara baada ya maji kujaa katika matenki yaliyopo shuleni hapo.

 

“Hatua tunazoenda kuchukua kwa sasa ni kufungua shauri polisi dhidi ya wahusika kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria ikiwa ni pamoja na kufanya mahesabu na kuandaa bili ya kiasi cha maji yaliyoibiwa kwa muda wote,” alisema Nachan.

Alipoulizwa juu ya madai ya wizi wa maji, Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Anna Mkapa, Sindato Seiya,  alikiri kufanyika wizi wa maji katika shule hiyo huku akitupia mpira kwa mlinzi na fundi wa miundombinu ya maji wa shule hiyo.

 

“Nimeiona sehemu yenyewe na toka jana usiku huyu fundi ametafutwa na hapokei simu hadi sasa maana yake anajua mwenyewe ni kitu gani amefanya.  Hapa shule kuna wafanyakazi wa asubuhi hadi saa tisa na anakabidhiwa shule mlinzi wa mchana ambaye pia anakabidhi kwa mlinzi wa usiku.  Hao ndio wanaweza kujua hili suala,”alisema Seiya.

 

Alisema yupo tayari kwa hatua zitakazochukuliwa kutokana na kwamba yeye anafahamu wamekuwa wakilipa bili za maji kwa njia ya hundi kila mwezi na kwamba wizi wa maji uliofanyika hajui wahusika wamefanya kwa faida ya nani.

Na Dixon Busagaga, Moshi. 

Comments are closed.