The House of Favourite Newspapers

Simba Ikishinda, Kila Mchezaji Kulamba Sh 4m

Kikosi cha timu ya Simba SC.

WACHEZAJI wa Simba wanaweza kutoka uwanjani wakiwa mamilionea leo ikiwa wataifunga Yanga kwenye mchezo wa ligi kuu utakaopigwa kwenye Uwanja wa Taifa.

 

Katika mchezo huo utakaopigwa saa 10 jioni, wachezaji wa timu hizo watakuwa na kazi moja tu ya kuhakikisha wanapambana uwanjani kuwania pointi tatu zitakazowaweka katika mazingira mazuri ya kutwaa ubingwa wa ligi kuu msimu huu.

 

Hata hivyo, kwa upande wa Simba ushindi huo utawawezesha wachezaji hao kujikusanyia mamilioni ya fedha kutoka kwa bilionea wa timu hiyo, Mohammed Dewji ‘Mo’ ambaye inadaiwa ametoa ahadi nono kwa wachezaji ikiwa watafanikiwa kuifunga Yanga.

Habari za kuaminika kutoka ndani ya Simba ambazo Championi Jumamosi limezipata zimedai kuwa, endapo watafanikiwa kuifunga Yanga katika mchezo huo fedha ambazo watapata hazitatofautiana sana na zile ambazo walipewa wakati walipotinga hatua ya makundi ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

Baada ya kutinga katika hatua hiyo wachezaji hao ambao walicheza katika mechi hiyo, kila mmoja alilamba kitita cha shilingi milioni nne (4,000,000).

 

“Kama wataibuka na ushindi kesho (leo) basi Sh 4,000, 000 zitamuhusu kila mchezaji, ni wajibu wao kupambana sasa kuhakikisha wanashinda ili waweze kupata kitita hicho ,” kilisema chanzo hicho cha habari.

 

Katika hatua nyingine, Kocha Mkuu wa Simba, Mbelgiji, Patrick Aussems amesema kila kitu kwa ajili ya mchezo huo kiufundi kipo vizuri na ni matumaini yake kuwa watapata ushindi.

 

“Tumejipanga vizuri kwa ajili ya mechi hiyo, ni matumaini yangu kuwa tutaibuka na ushindi, kwa hiyo niwaombe tu wapenzi na mashabiki wetu wajitokeza kwa wingi uwanjani kuja kutuunga mkono,” alisema Aussems.

Comments are closed.