Simba Queens, Yanga Princess Kukiwasha Mo Arena Leo
MAKOCHA wa Simba Queens na Yanga Princess, kila mmoja ametamba kumfunga mwenzake katika dabi yao kali itakayopigwa leo Jumamosi pale Simba Mo Arena jijini Dar.
Simba Queens wanaingia katika mchezo huo wa Ligi Kuu ya Wanawake wakiwa na kumbukumbu ya kuwachapa JKT Queens mabao 3-0 wakati Yanga Princess walitoka kuwafunga Mlandizi Queens mabao 2-0.
Rekodi za dabi hiyo tangu ilipoanza kupigwa msimu wa 2018/19 inaonyesha kuwa Yanga hawajawahi kushinda kwani kila walipoingia waliambulia vichapo kutoka kwa Simba.
Msimu wa 2018/19, Simba Queens walishinda 7-0 na 5-1 kisha wakaendeleza kilio kwa kuwapiga Yanga 3-1 na 5-1 msimu wa 2019-2020.Kocha Mkuu wa Yanga Princess, Edna Lema ‘The Special One’ aliliambia Championi Jumamosi kuwa:
“Huu ni msimu wangu wa kuonyesha ubora wangu, nataka kuwaonyesha watu kuwa nina uwezo wa kuwafunga Simba na kuchukua ubingwa.
“Lengo hasa ni kuwa bingwa msimu huu na ili kuwa bingwa lazima uzifunge timu ngumu na bora kwenye ligi.
Tuombe Mungu vijana wawe salama tu.”Naye Kocha wa Simba Queens, Mussa Hassan Mgosi, alisema: “Kwa upande wetu maandalizi yamekaa sawa kabisa na tunasubiri wakati ufike, Yanga hawana uwezo wa kutufunga, labda watachofanya ni kupunguza idadi ya mabao kutoka kufungwa 7-0 hadi 4-0, lakini siyo kutufunga, hiyo haitakuja itokee.
Stori: ISSA LIPONDA,Dar es salaam | Championi Jumamosi