The House of Favourite Newspapers

Simba vs Coastal…Rekodi Mpya Inawekwa

0

REKODI mpya inakwenda kuwekwa leo Jumapili kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar pindi Simba itakapoikaribisha Coastal Union ukiwa ni mchezo wa Ligi Kuu Bara.

 

Mchezo huo wa kiporo, unatarajiwa kuanza saa 1:00 usiku ambapo Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), imesema, endapo Simba itapata ushindi au sare, basi wataitambua rasmi kama bingwa wa ligi hiyo kwa msimu wa 2020/21 na kuweka rekodi ya ubingwa wa nne mfululizo licha ya kwamba tayari kimahesabu ni bingwa.

 

Ofisa Habari wa TPLB, Kareem Boimanda, alisema: “Kimsingi au kikanuni ipo hivi, kama Simba watapata alama yoyote kesho (leo) dhidi ya Coastal Union ni wazi watatangazwa kuwa mabingwa kwa kuwa hakuna timu nyingine ambayo itaweza kupata alama zake kwenye michezo iliyosalia.”

 

Simba ina alama 76, ikongoza ligi hiyo baada ya mechi 31 ikisaliwa na tatu, inafuatiwa na Yanga yenye alama 70 ilizozipata kwa kucheza mechi 32.

Imebakiwa na mbili ambazo ikishinda zote, itaishia alama 76.Wakati kikanuni Simba wakijiandaa kutangazwa mabingwa rasmi leo, Coastal wamegoma kuwa daraja la kutokea tukio hilo ambapo Kocha Msaidizi, Joseph Lazaro, alisema:

 

“Hautakuwa mchezo rahisi kwa sababu tumekuja kupambana ili kujinasua kwenye mtego tuliopo, hatutapenda kuona Simba wanatufanya sisi daraja la ubingwa wao.”Kwa upande wa Kocha Msaidizi wa Simba, Seleman Matola, alisema:

 

“Nafikiri kila Mwanasimba anatamani kuona tunatangazwa rasmi kuwa mabingwa. Mchezo huu ni muhimu sana na haitakuwa rahisi, ila naamini ushindi utapatikana mapema tu.”Coastal Union wanahitaji ushindi ili wajinasue kwenye janga la kushuka daraja ambapo hivi sasa wana alama 34, wakishika nafasi ya 17 baada ya kucheza mechi 31.

 

Rekodi zinaonesha kwamba, kuanzia msimu wa 2013/2014 hadi sasa, timu hizo zimekutana mara 11, huku mara mbili Simba ikiibuka na ushindi mnono ikifanya hivyo mzunguko wa kwanza msimu huu iliposhinda 7-0, pia msimu wa 2018/2019, ilishinda 8-1.

 

Katika mechi hizo 11, Coastal Union imefanikiwa kuibuka na ushindi mara moja tu ikiwa ni msimu wa 2013/2014 iliposhinda 1-0.

 

Simba yenyewe imeshinda jumla ya mechi sita, huku sare zikiwa nne.Coastal Union leo inausaka ushindi wake wa kwanza mbele ya Simba baada ya kupita miaka saba, huku Simba ikitaka kuendeleza rekodi yao ya ushindi dhidi ya wapinzani wao hao

Leave A Reply