The House of Favourite Newspapers

Simba Waitaja Yanga Kipigo Ligi Ya Mabingwa

0

BAADA ya Simba kutupwa nje katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya kwanza na kuangukia Kombe la Shirikisho Afrika, inaelezwa uongozi wa timu hiyo umewanyooshea vidole wapinzani wao Yanga kuwa ndiyo wamechangia hali hiyo.

 

Simba imeshindwa kufuzu hatua ya makundi baada ya sare ya jumla ya maba0 3-3 dhidi ya Jwaneng na kuondoshwa kwa bao la ugenini.

 

Juzi Jumapili, Simba ilikubali kichapo cha mabao 3-1 na kufungashiwa virago jambo ambalo wenyewe wanaamini walihujumiwa na Yanga.

Kwa mujibu wa taarifa ambazo Spoti Xtra limezipata, zinasema kuwa benchi la ufundi pamoja na uongozi wa Simba umekuwa ukiwalaumu Yanga kuwa ndiyo sababu kubwa iliyopelekea kupoteza mchezo huo kutokana na kuwapokea wapinzani wao na kuwaonesha njia za kupita kabla ya mchezo huo.

 

“Kiukweli hadi sasa hatuelewi nini kimepelekea kupoteza ule mchezo, yaani hakuna ambaye yupo sawa kwa kuwa hatujui wapi tulikosea maana tulicheza vizuri na kutengeneza nafasi nyingi.

“Lakini ukiondoa hayo, Yanga nao wamechangia kwa sababu baadhi ya watu walikuwa wakisema kwamba ndiyo wamewapokea wale wapinzani wetu, tena wamewaweka pale White Sand karibu na ilipo kambi yetu.

 

“Pia baada ya mchezo baadhi ya watu wakubwa wa Yanga walienda pale hotelini kwa wapinzani wetu kuonana na wachezaji,” alisema mtoa taarifa huyo.

 

Spoti Xtra lilimtafuta Kocha Msaidizi wa Simba, Hitimana Thiery ambaye alisema hajui kitu gani anaweza kueleza kwa kuwa matokeo yameshatokea.

 

Kwa upande wa Yanga, Spoti Xtra lilizungumza na Ofisa Mhamasishaji, Haji Manara kuhusu tuhuma wanazopewa ambapo alisema leo Jumanne wataweka wazi kila kitu juu ya jambo hilo ikiwemo kuzungumzia mchezo wao ujao dhidi ya Azam.

STORI: IBRAHIM MUSSA NA MUSA MATEJA, Dar

Leave A Reply