The House of Favourite Newspapers

Simba ‘Wapapaswa’ na Ruvu Shooting

0

Timu ya Simba imekubali kufungwa  kwa mara ya pili mfululizo kwenye Ligi Kuu ya Vodacom,  kwenye Uwanja wa Uhuru kwa kichapo cha 1-0 dhidi ya Ruvu Shooting na kuzua  sintofahamu licha ya vijana wa Mkwasa kuwa  pungufu  baada ya mchezaji wao kupata kadi nyekundu.

 

Simba wamepoteza tena  ikiwa ni siku chache tu kupigishwa gwaride  na Prisons ya Mbeya, na kuzua gumzo kwa wadau na mashabiki wakihoji nini kinaendelea ndani ya msimbazi licha ya Majeruhi walionayo lakini bado timu haichezi vizuri.

 

Mfungaji pekee wa goli la Leo kwa upande wa Ruvu Shooting alikuwa Fully Zully Maganga dakika ya 36, Simba walipata Penati dakika ya 80 ambayo nahodha John Bocco aliikosa na kuzamisha matumaini ya mnyama kuondoka angalau na pointi moja.

 

Aidha kwenye mchezo huo Ruvu shooting walicheza pungufu baada ya Shabani Msala kutolewa kwa kadi nyekundu dakika ya 75, baada ya kumfanyia madhambi Luis Miquisson.

 

Kwa matokeo hayo  Azam anaendelea kusalia kileleni mwa msimamo na pointi 21, baada ya michezo nane, Yanga anafuatia na pointi 19 imeshuka dimbani mara saba, Biashara United nafasi ya tatu na pointi 16 akicheza mechi nane na bingwa mtetezi Simba nafasi ya nne na pointi 13 akishuka dimbani mara nane.

Leave A Reply