The House of Favourite Newspapers

Simba Yaachana na Morrison, Chikwende Atua

0
Mghana, Bernard Morrison.

INAELEZWA kuwa uongozi wa Simba umepanga kuachana na nyota wa timu hiyo, Mghana, Bernard Morrison kufuatia madai ya kiungo huyo kusumbuliwa na ugonjwa wa hernia ‘Ngiri Maji’ huku nafasi yake ikitarajiwa kuchukuliwa na kiungo mshambuliaji mpya wa timu hiyo, Mzimbabwe, Perfect Chikwende.

 

Simba imefikia hatua ya kuchana na Morrison aliyejiunga na Simba kwa mkataba wa miaka miwili kutokana na tatizo la ugonjwa huo unaodaiwa kumuweka nje kwa muda wa miezi sita ikiwa atafanyiwa upasuaji, kitu ambacho Simba hawataweza kukivumilia kwa kuwa wanashiriki Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

Kabla ya usajili wa Chikwende, Simba tayari ilikuwa na wachezaji kumi wanaotakiwa kwa mujibu wa kanuni za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) za kuruhusu kila timu kusajili idadi hiyo ya wageni, ambao ni Bernard Morrison, Pascal Wawa, Chris Mugalu, Larry Bwalya, Luís Miquissone, Meddie Kagere, Joash Onyango, Clatous Chama, Taddeo Lwanga na Francis Kahata kabla ya juzi kumalizana na Chikwende kwa mkataba wa miaka miwili akitokea FC Platinum ya Zimbabwe.

Bernard Morrison

Kwa mujibu wa taarifa ambazo Championi Jumamosi limezipata kutoka ndani ya uongozi wa Simba, tayari uongozi wa timu hiyo umeshakaa na kiungo huyo kwa kufanya mazungumzo ya kuvunja mkataba wake ili nafasi yake ichukuliwe na Chikwende kutokana na madai ya kusumbuliwa na ugonjwa wa hernia.

 

“Morrison amekutana na uongozi wa Simba juu ya suala la yeye kuvunjiwa mkataba wake kutokana na kusumbuliwa na tatizo la ugonjwa wa hernia, kwa sababu anatakiwa kufanyiwa upasuaji ambao utamuweka nje kwa muda wa miezi sita.“

 

Bado Simba wanafanya naye mazungumzo ya kuvunja mkataba wake kwa pande zote mbili kufikia makubaliano mazuri kwa sababu nafasi yake Morrison itachukuliwa na Perfect Chikwende ambaye ameshamalizana na uongozi,” alisema mtoa taarifa.

Perfect Chikwende

Juzi baada ya mechi kati ya Simba na Yanga ambayo iliisha kwa vijana wa Jangwani kushinda kwa penalti 4-3 katika fainali ya Mapinduzi, Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Simba, Kassim Dewji alisikika akizungumzia afya ya Morrison baada ya wadau kuhoji sababu ya kumfanya asicheze, aliwajibu:

 

“Wewe unayelalamika, unataka Morrison acheze, unajua Morrison anamatatizo gani?… Hujui? Morrison ana hernia kwa hiyo hawezi kukimbia wala hawezi kucheza na mpaka afanyiwe oparesheni kwa hiyo sasa hivi yupo na timu lakini hawezi kucheza“

 

Umemuona anacheza mechi yoyote, umemuona anafanya mazoezi zaidi ya kufanya mazoezi mepesi tu kwa sababu anatatizo la hernia, wamejaribu kuangalia kama itaweza kutibika ikishindikana afanyiwe operesheni.

 

Sasa hivi imeamuliwa afanyiwe operesheni, akifanyiwa oparesheni miezi sita hachezi,” ilisikika sauti ya Kassim Dewji akimjibu mmoja ya wadau waliouliza kutocheza kwa kiungo huyo.

USAJILI YANGA: MTAMBO wa MABAO Alivyotua AIRPORT KIMYA KIMYA, PACHA wa NTIBAZONKIZA..

Leave A Reply