The House of Favourite Newspapers

Simba Yafuzu Hatua Ya Makundi, Dilunga Atupia

0

KIKOSI cha Simba kinachonolewa na Kocha Mkuu, Pablo Franc leo Desemba 5 kimefanikiwa kuandika historia mpya kwenye Kombe la Shirikisho baada ya kuweza kufuzu hatua ya makundi.

 

Kwenye mchezo wa leo uliochezwa Uwanja wa Heroes,Zambia dakika 90 zimekamilika kwa ubao kusoma Red Arrows 2-1 Simba ambapo bao la Simba lilipachikwa na kiungo mzawa Hassan Dilunga.

 

Dilunga aliweza kupachika bao hilo akiwa ndani ya 18 baada ya beki wa Red Arrows kufanya uzembe kwenye kuokoa mpira mrefu uliopigwa na kiungo Mzambia, Rarry Bwalya ilikuwa dakika ya 67.

 

Mabao ya Red Arrows ambao walikuwa bora kwenye mipira ya juu yalifungwa na Eric Banda dakika ya 44 kwa shuti kali na lile la pili lilifungwa na Joesph Phiri dakika ya 46 kwa kichwa kilichowashinda mabeki.

 

Simba ina kazi kubwa hatua ya makundi hasa kufanya maboresho eneo la ulinzi pamoja na ushambuliaji kwa kuwa wameshindwa kutumia nafasi ambazo wamezipata huku mabeki wakiwa na mwendelezo wa kukaba kwa macho.

 

Simba inasonga mbele kwa jumla ya mabao 4-2 kwa kuwa mchezo wa kwanza uliochezwa Uwanja wa Mkapa Simba ilishinda mabao 3-0 ambayo yalifungwa na Bernard Morrison aliyetupia mawili lakini leo alibanwa na wapinzani wake pamoja na Meddie Kagere huyu alitupia bao moja.

Leave A Reply