Simba Yaiwekea Al Ahly Kikao Kizito
MIKAKATI ya kuhakikisha Simba inavuna pointi tatu dhidi ya Al Ahly ya Misri, imeendelea usiku wa kuamkia jana, ambapo benchi la ufundi la timu hiyo na uongozi wa wa juu, ukiongozwa na Mtendaji Mkuu, Barbara Gonzalez, ulikaa kikao kizito kujadili namna watakavyoikabili timu hiyo.
Keshokutwa Jumanne, Simba itakuwa mwenyeji wa Al Ahly kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam, ukiwa mchezo wa hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.Timu hizo zimepangwa Kundi A sambamba na AS Vita na Al-Merrikh.
Katika mechi zao za kwanza, Simba na Al Ahly zote zilianza kwa ushindi. Chanzo chetu kutoka ndani ya Simba, kimelidokeza Spoti Xtra kwamba, usiku wa kuamkia jana Jumamosi, benchi la ufundi na viongozi wa juu walikaa kikao na kupeana majukumu ya kufanya.
“Kuelekea mechi yetu na Al Ahly, tayari sisi kama benchi la ufundi tumekaa kikao na uongozi wetu kisha tukagawana majukumu ya kufanya ili kuhakikisha tunapata ushindi muhimu hapa nyumbani.“
Baadhi ya masuala tuliyojadili ilikuwa ni pamoja na kuhakikisha tunatengeneza saikolojia za wachezaji, lakini pia kocha mkuu amepata mbinu za kuwashinda wapinzani wetu,” kilisema chanzo.
Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa Simba, Haji Manara, alizungumzia maandalizi ya mchezo huo kwa kusema: “Tayari maandalizi yako safi, tunaahidi ushindi mbele ya Al Ahly.
“Tutaingia kwa tahadhari kubwa kwa sababu tunawaheshimu wapinzani wetu ni timu kubwa na ni mabingwa wa Afrika, ila na wao wanafahamu kuwa wanakutana na mabingwa wa Tanzania, hivyo ushindi ni lazima.”
STORI NA MATEJA MUSA | GPL