The House of Favourite Newspapers

Simba yampa Tambwe milioni 14 kimyakimya

0

AmissTambwe2

Mshambuliaji wa Yanga, Amissi Tambwe.

Khadija Mngwai,Dar es Salaam
MSHAMBULIAJI wa Yanga, Amissi Tambwe, ameyakomba mamilioni ya Simba baada ya uongozi wa timu hiyo kukamilisha malipo yake ya zaidi ya shilingi milioni 14 aliyokuwa akidai baada ya kukatisha mkataba wake msimu uliopita.

Tambwe aliachwa Simba katika msimu uliopita kwenye dirisha dogo kufuatia kudaiwa kuwa, aliyekuwa kocha wa timu hiyo Patrick Phiri alimkataa katika kikosi chake kwa madai ya kushindwa kuendana na mfumo wake. Hata hivyo, Phiri alikanusha, akidai viongozi wenyewe ndiyo waliomkataa.

Mchezaji huyo ambaye amefunga mabao manne kwenye ligi hadi sasa, alikuwa akiidai Simba dola elfu 7,000 ambazo ni zaidi ya shilingi milioni 14 kufuatia kukatishwa kwa mkataba wake wa miezi sita ambapo alikuwa akilipwa mshahara wa milioni moja na nusu kwa mwezi.

Akizungumza na Championi Jumatano, Tambwe amesema kuwa, tayari ameshamalizana na Simba kwa kumlipa fedha zake zote kupitia mapato ya mlangoni, japokuwa ilikuwa tabu sana kupata malipo hayo.

“Ni kweli tayari nimeshamalizana na Simba kwa kunilipa fedha zangu zote nilizokuwa nikiwadai kutokana na kunikatishia mkataba wangu, japokuwa ilikuwa mbinde kunipa.

“Kwa sasa siidai klabu hiyo na ninachoangalia ni jinsi gani naweza kuisaidia timu yangu ya Yanga iweze kufanikiwa kufanya vyema na hatimaye kutetea ubingwa wetu,” alisema Tambwe.

Leave A Reply