Kikosi cha timu ya Yanga wakifamnya maombo na kocha wao.
Na Khadija Mngwai, Championi Jumamosi, 23.12.2016 Toleo No. 1949
HATIMAYE Simba, Yanga na Azam FC zimemalizana na Idara ya Uhamiaji kwa kuwalipia vibali vya kufanya kazi nchini wachezaji na watendaji wake wengine klabuni.
Siyo klabu hizo tu, hata African Lyon nayo jana kabla ya saa 7:00 mchana ilikuwa imekamilisha taratibu zote za uhamiaji kwa wachezaji wake wa kigeni.
Awali Idara ya Uhamiaji ilizipiga mkwara klabu za Ligi Kuu Bara kutowatumia wachezaji na watendaji wake wengine ambao ambao hawajatimiza taratibu za uhamiaji ikiwemo kupewa kibali cha kufanya kazi nchini.
Kikosi cha timu ya Simba.
Uhamiaji ilitoa muda hadi kufikia jana saa 7:00 mchana klabu hizo ziwe zimekamilisha utaratibu wa kuwasilisha vibali vya makazi na vya kazi kwa watendaji hao jambo lililotekelezwa na timu hizo.
Akizungumza na Championi Jumamosi, Ofisa wa Uhamiaji wa Mkoa wa Dar es Salaam, John Msumule alisema klabu zote za mkoa wake ikiwemo African Lyon zimekamilisha taratibu zote hivyo zinawaruhusiwa kuwatumia wachezaji na makocha wao.
“Nilitoa muda hadi leo (jana) saa 7:00 mchana klabu zote ziwe zimekamilisha taratibu zote za vibali kwa makocha na wachezaji wao na iwapo wasingekamilisha basi wasingeruhusiwa kufanya kazi.
“Klabu zote zimekamilisha zoezi hilo ikiwemo African Lyon, nimesimamia zoezi hili kwa upande wa mkoa wangu hivyo iwapo kuna wachezaji wa mikoa mingine ambao hawana vibali sijui,” alisema Msumule.
Kwa mujibu wa Msumule, kibali cha ukaazi ni dola 2,050 kwa mwaka sawa na Sh milioni nne na kile cha kufanyia kazi dola 1,000 kwa mwaka sawa na Sh milioni mbili.
Waliolipiwa kwa upande wa Simba ni wachezaji Javier Bokungu, Goue (Fredrick) Blagnon, Laudit Mavugo, Daniel Agyei, James Kotei na Method Mwanjale huku makocha wakiwa ni Kocha Mkuu Joseph Omog, Kocha Msaidizi Jackson Mayanja na Kocha wa Makipa Idd Salim.
Kwa upande wa Yanga, waliolipiwa ni Kocha Mkuu George Lwandamina, Mkurugenzi wa Ufundi, Hans van Der Pluijm, Kocha wa Viungo, Noel Mwandila na wachezaji ni Donald Ngoma, Haruna Niyonzima, Amissi Tambwe, Vincent Bossou, Justine Zulu, Thabani Kamusoko na Obrey Chirwa.
Aidha, baadhi ya wachezaji ambao vibali vyao vilikuwa bado ni pamoja na Donald Ngoma, Laudit Mavugo, Amissi Tambwe, James Kotei na kwa upande wa makocha wote wa timu hizo za Simba, Yanga na Azam.
Kwa mujibu wa Msumule, Yanga ilikuwa imelipa baadhi ya vibali vya makazi bila ya vya kazi lakini Simba haikuwa imelipa kibali chochote kwa watendaji wake.
Comments are closed.