The House of Favourite Newspapers

St Mary Goreti Yapongezwa Na Serikali Kwa Ubunifu Kuelekea Jubilee

0
Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Mh. Kisare Makori (katikati) akishuhudia Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari ya St Mary Goreti, Sr Clementina Kachweka (kulia) akipokea Lipa Namba ya Tigo itakayotumika kupokea michango kwa ajili ya harambee ya shule hiyo, kutoka kwa Meneja Mauzo wa Tigo, Silas Mkuyu (wa pili kushoto). Wengine kutoka kushoto ni Meneja Msaidizi wa shule, Moses Silayo na Mwenyekiti wa Bodi, Injinia Theonis Bebwa.

SERIKALI mkoani Kilimanjaro imeupongeza uongozi wa shule ya sekondari ya St Maria Goreti iliyoko Moshi, kwa ubunifu na juhudi katika kuboresha na kutunza mazingira sambamba na kuboresha afya ndani ya jamii.

Pongezi hizo zimetolewa mwishoni mwa wiki na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Bw Nurdin Babu katika taarifa iliyosomwa kwa niaba yake na Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Bw Kisare Makori, wakati wa hafla ya uzinduzi wa harambee ya maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa shule hiyo.

“Mbali na kazi nzuri mnayofanya katika kutoa elimu ambayo imebadilisha maisha ya watu wengi, pia taarifa zinaonyesha ya kuwa mmetoa na mnaendelea kutoa michango mingi katika kuboresha mazingira na afya ndani ya jamii, hili hatuna budi kuwapongeza”, alisema na kuongeza kwa kufanya yote hayo shule hiyo inaunga mkono juhudi za Serikali za kujenga jamii iliyo bora kielimu na kiafya.

Aliongeza, “Juhudi zenu hizi hazina budi kuungwa mkono na wadau wengine kutokana na ukweli ya kuwa elimu na afya njema ni muhimu kwa wanadamu ambao wana kazi ya kukabiliana na changamoto za kimaisha kila siku”.

Bw Babu pia alipongeza taasisi za Kidini kwa michango inayotoa kupitia sekta mbalimbali zikiwemo za elimu na afya jambo ambalo alisema limechangia wananchi wengi kupata huduma nzuri na endelevu kupitia taasisi hizo.

“Mfano mzuri ni nyinyi wa shule ya St Mary Goreti ambao mmeamua kuweka programu ya kuboresha mazingira kwa kupanda miti kama sehemu ya maadhimisho ya jubilee yenu; uamuzi huu mmeuchukua muda muafaka haswa ikitiliwa maanani ya kuwa maboresho ya mazingira ni agenda muhimu ambayo inapewa kipaumbele kikubwa na Serikali katika kipindi hiki”, alisema.

Bw. Babu alitoa rai kwa wadau mbalimbali wa maendeleo na wanachi wote kwa ujumla kutoa ushiriakiano wao wa dhati kwa uongozi wa shule ya sekondari ya Maria Goreti ili kufanikisha sherehe yao.

“Nina uhakika kuna wadau wengi huko nje ikiwemo wote waliosoma katika shule hii na pindi tu wakiskia taarifa hizi, watajitokeza kuchangia kw anguvu zote,” alisema.

Katika taarifa yake Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Maria Goreti Sr Clementina Kachweka alisema maadhimisho hayo ya miaka 25 tangu kuanizhswa kwa shule hiyo yantarjiwa kufanyika Septemba, mwakani.

“Kuelekea maadhimisho hayo tunatarajia kufanya ukarabati mkubwa na ndiyo haswa sababu ya uzinduzi rasmi wa Harambee ili kupata fedha kwa ajili ya shughuli za ukarabati huo”, alisema huku akipokea Lipa Namba ya mtandao wa Tigo ambayo ni moja ya njia zitakazotumika kutuma michango.

Alisema Lipa namba ya Tigo ni 7945925 na kwa watakaotaka kuweka moja kwa moja benki ni kupitia akaunti ya CRDB 0152628700800.

Aliongeza, “Pia kuelekea jubilee tumeandaa shughuli malimbali ambazo tutazifanya kama shule kwa kushirikiana na jamii kwa ujumla, ambazo ni pamoja na upandaji miti kwa ajili ya kutunza vyanzo vya maji; hili pia litakuwa ni kuunga mkono ofisi yako ambayo imekuwa mstari wa mbele katika kutunza mazingira”.

Alizitaja shughuli nyingine kuwa ni pamoja na kuwa na kampeni ya afya kwa kuachangia damu na matembezi ya hisani yatakayolenga kukusanya fedha kwa ajili ya shughuli zinazohusiana na maadhimisho hayo.

“Matarajio yetu ni kukusanya jumla ya shilingi milioni 600 kwa ajili ya ukarabati wa shule yote kwa ujumla; tayari kwa kuanzia tumeshawaarifu wazazi wenye wanafunzi wanaosoma shuleni hapa kuhusu mipango yetu hii”, alisema na kuongeza, ni matumaini yetu watatupa ushirikiano wa kutosha ili tuweze kufikia malengo yetu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya shule hiyo Mhandisi Theonis Bebwa, aliishukuru Serikali ya Mkoa kwa ushirikiano inaotoa kwa shule hiyo mara kwa mara ambao alisema pia umechangia mafanikio ya shule hiyo.

Aidha alielezea matumaini yake ya kuwa uongozi wa Bodi na ule wa shule hiyo utapata ushirikiano mkubwa kutoma kwa wanafunzi waliosoma shuleni hapo ambao alisema ni zaidi ya 10,000 walioko ndani na nje ya nchi, jambo amalo alisema litafanikisha shughuli hizo za jubilei.

Shughuli hizi za kuelekea jubilee ya St Mary Goreti zinaratibiwa na Executive Solutions Limited moja ya makampuni yanayoongoza katika kuandaa matukio na kuratibu maswala ya habari na mawasiliano.

Leave A Reply