The House of Favourite Newspapers

Stars Yalazimisha Sare Dhidi ya Tunisia

0

 

TIMU ya taifa  (Taifa Stars)  usiku jana  Novemba 17, 2020,  imeshindwa kuiutumia vyema faida ya kucheza nyumbani baada ya kulazimisha sare ya  1-1 dhidi ya Tunisia kwenye mchezo wa kundi  J wa kufuzu kwa Kombe la Mataifa Huru ya Afrika (AFCON) ambayo fainali zake zitachezwa mwakani nchini Cameroon.

 

Mchezo wa leo ambao ulikuwa ni muhimu kwa Stars kushinda kwa kuwa ule wa kwanza ugenini ilikubali kupoteza kwa kufungwa bao 1-0 nchini Tunisia, ulikuwa mgumu kwa Stars kwa kuwa walikubali kufungwa kipindi cha kwanza.

 

Wageni walianza mchezo kwa kasi na kufanikiwa kupata goli la kuongoza mapema tu dakika ya 11, likifungwa  na Saif-Eddine Khaoui  na kuwanyamazisha mashabiki waliohudhuria mtanange huo kwenye dimba la Mkapa.

 

Uamuzi wa kumtoa Himid Mao Mkami na kuingia kwa Feisal Salum kipindi cha ulionekana wenye tija  kwani haikumchukua muda mrefu ya kiungo huyo  kuonyesha uwepo wake uwanjani, baada ya kutandika mkwaju mkali uliomshinda mlinda mlango na kutinga nyavuni na kuisawazishia Stars,  kwenye dakika 48 kipindi cha pili.

 

Pointi hiyo moja inaifanya Stars iwe nafasi ya tatu ikiwa na pointi nne baada ya kucheza mechi nne huku Tunisia ikiwa nafasi ya kwanza na pointi 10.

 

Nafasi ya nne ipo mikononi mwa Libya yenye pointi tatu na ile ya pili ni mali ya Equatorial Guinea yenye pointi 6 kwenye kundi J.

Leave A Reply