The House of Favourite Newspapers

Straika Stars Mtegoni Yanga

KATIKA kukiimarisha kikosi chake, Kaimu Kocha Mkuu wa Yanga, Charles Boniface Mkwasa, ameomba mchezo mmoja wa kirafiki watakaocheza dhidi ya Coastal Union ya mkoani Tanga anayoichezea straika wa timu ya taifa, Taifa Stars, Ayoub Lyanga anayetajwa kuwa kwenye mipango ya usajili wa dirisha dogo.

 

Ligi Kuu kwa sasa imesimama kwa muda wa wiki mbili kupisha michezo ya kimataifa ambapo kwa Tanzania itakuwa ikiwania kufuzu Afcon 2021.

 

Wiki iliyopita Mkwasa alikabidhiwa rasmi mikoba ya kukinoa kikosi hicho akikaimu nafasi ya Mkongomani Mwinyi Zahera aliyesitishiwa mkataba wake kwa kile kilichotajwa matokeo mabaya. Akizungumza na Championi Ijumaa, Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa Yanga, Hassan Bumbuli alisema kuwa mchezo umepangwa kuchezwa keshokutwa Jumapili jioni kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam, ikiwa ni moja ya mipango ya kujiweka fiti katika mechi za ligi.

 

Bumbuli alisema kuwa Mkwasa atautumia mchezo huo kama sehemu ya kuangalia uwezo wa kila mchezaji na kutengeneza kikosi kitakacholeta ushindani katika ligi lakini itakuwa changamoto kwa Lyanga ambaye kama akionyesha uwezo wa juu anaweza kuwashawishi mabosi wa Yanga ili wamsajili.

 

Aliongeza kuwa mara baada ya kocha huyo kuomba mchezo huo, haraka mabosi wamekubali kumpatia kwa lengo la kusuka kikosi imara kitakachowapa matokeo mazuri ya ushindi katika kipindi hicho ambacho hakuna kocha mkuu. “Mara baada ya kumaliza mchezo wa ligi kuu na Ndanda FC ambao tuliibuka na ushindi wa bao 1-0, wachezaji walipewa mapumziko ya siku tano kabla ya leo (jana) kuanza mazoezi ya pamoja.

 

“Baada ya mapumziko hayo kocha aliomba viongozi mchezo mmoja wa kirafiki ambao tutacheza dhidi ya Coastal, lakini kabla ya kucheza na hao tulipanga kucheza na Ruvu Shooting, lakini ilishindikana. “Wachezaji wote wapo fiti na kila mmoja anaonyesha morali ya juu ambapo benchi la ufundi litatumia muda huu kuhakikisha wanayafanyia kazi baadhi ya makosa yaliyojitokeza nyuma.

 

Yanga inashika nafasi ya 15 katika msimamo wa ligi kuu ikijikusanyia pointi 10 kati ya mechi tano walizocheza, wakishinda michezo mitatu, sare mmoja, huku wakifungwa mmoja na Ruvu.

Comments are closed.