The House of Favourite Newspapers

Straika Zesco Avujisha Siri Yanga

Straika wa zamani wa Zesco, Maybin Kalengo.

BENCHI la Ufundi la Yanga lililo chini ya Kocha Mkuu Mkongomani, Mwinyi Zahera, limepanga kumtumia straika wa zamani wa Zesco, Maybin Kalengo kuwamaliza wapinzani wao.

 

Kalengo ni kati ya washambuliaji wa Yanga waliojiunga na timu hiyo kwenye msimu huu akitokea Zesco.

Yanga inatarajiwa kucheza mchezo wake wa raundi ya kwanza wa Ligi ya Mabingwa Afrika Jumamosi hii kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

 

Akizungumza na Championi Jumatano, Zahera alisema kuwa tayari wameshawamaliza wapinzani wao hao kabla ya mchezo huo kutokana na kujua mbinu, mfumo na wachezaji hatari wa kuwazuia.

 

Zahera alisema wamemtumia straika huyo na baadhi ya marafiki zake kwa ajili ya kuwajua wapinzani wao, hivyo hana hofu ya mchezo huo, kikubwa mashabiki wajitokeze kwa wingi katika mchezo huo kwa ajili ya kuwasapoti wachezaji wake.

Maybin Kalengo mwenye jezi namba 19 akiwa mazoezini.

Aliongeza kuwa straika wake huyo anaifahamu vizuri Zesco aliyokuwa anaichezea kabla ya kutua Yanga, hivyo wanamtumia yeye kuzijua mbinu wanazozitumia kwenye mechi za nyumbani na ugenini.

 

“Sina hofu ya mchezo wetu dhidi ya Zesco, licha ya kuifahamu vizuri, lakini tunachotakiwa kukifanya ni kuzisoma mbinu na kuwajua wachezaji hatari wa kuchungwa mara tutakapokutana nao.

 

“Uzuri ni kwamba mimi tayari nimeshamaliza katika hilo, kwani yupo Kalengo ambaye anaunda safu ya ushambuliaji katika timu yangu aliyetokea Zesco katika msimu huu.

 

“Yeye anazifahamu mbinu zao zote ambazo tayari nimezijua, pia nimewatumia marafiki zangu wa karibu katika kuwasoma wapinzani wetu kama unavyofahamu niliwahi kufundisha Zambia Klabu ya Buildcon, hivyo sina hofu, kikubwa mashabiki wajitokeze kwa wingi kuisapoti timu yao,” alisema Zahera.

 

Comments are closed.