Sven Afungukia Benchi la Ajibu Simba
SVEN Vandenbroeck ambaye ni Kocha Mkuu wa Simba, amefunguka kwamba idadi kubwa ya wachezaji ambao wana uwezo wa kushambulia ndiyo sababu ambayo inawafanya baadhi ya wachezaji wake kukosa nafasi ya kucheza akiwemo Ibrahim Ajibu.
Kocha huyo ameongeza kuwa, eneo hilo ndilo ambalo limekuwa likimpa mawazo pale ambapo analipanga kutokana na idadi yake kuwa kubwa ambapo kila mchezaji amekuwa akionyesha uwezo wa juu.
Ajibu kwa msimu huu amefanikiwa kucheza mechi moja dhidi ya Ihefu, huku akikaa benchi kwenye mechi dhidi ya Mtibwa Sugar, Biashara United na Gambina FC.
Wachezaji wengine wanaocheza eneo la ushambuliaji la Simba ambao hawajapata nafasi katika Ligi Kuu Bara ni Charles Ilanfya, Miraji Athuman ‘Sheva’ na Hassan Dilunga.
Kocha huyo ameliambia Spoti Xtra kuwa, suala hilo la kuwa na wachezaji wengi ambao wana uwezo mkubwa ndilo ambalo linamfanya baadhi yao hadi sasa washindwe kuingia kwenye kikosi cha kwanza.
“Kuna washambuliaji wengi ndani ya kikosi, kuna changamoto kubwa eneo la ushambuliaji na hata ninapowapanga kuna wengine hawatumiki.
“Kila mmoja anatakiwa apambane kwa ajili ya kupata nafasi na unajua kwenye mechi nafasi ni chache ndiyo maana unaona wengine wameishia benchi bila ya kutumika kabisa, siyo kama hawana uwezo,” alimaliza Sven.
SAID ALLY, Dar es Salaam