KOCHA Mkuu wa Simba, Sven Vandenbroeck, amesema kuwa anasikitika kuwa kiungo wake raia wa Brazil, Gerson Fraga, hatakuwa sehemu ya kikosi kitakachocheza michezo ya awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Plateau ya Nigeria kutokana na majeraha yake.
Sven alisema alikuwa ameshapanga namna ya kumtumia Fraga kwenye mashindano hayo makubwa Afrika kwa sababu ni aina ya wachezaji ambao wanajua nini wafanye katika wakati gani na ni mtu ambaye anapambana kwa dakika zote 90.
Akizungumza na Championi Jumatano, Sven alisema ni hasara kubwa kumkosa Fraga kwenye kipindi hiki cha mashindano ya kimataifa kwa sababu kiungo huyo wa chini, alishaingia kwenye mfumo wake na alishampangia majukumu ya kufanya kwenye michezo hiyo kutokana na uzoefu wake.
“Ni hasara kubwa sana kumkosa mtu kama Fraga kwa sababu ni mchezaji ambaye anajua nini afanye akiwa uwanjani. Ni mpambanaji na anayejituma wakati wote uwanjani, alishaingia kwenye mfumo wangu na nilishapanga majukumu yake kwenye michezo ya kimataifa.
“Bahati hatutakuwa naye kwa sasa, hasara kwetu na inatakiwa tutafute mbadala wake kwa haraka kama ambavyo inafahamika,” alisema Sven. Fraga aliondoka nchini mwezi uliopita na kurejea kwao Brazil baada ya kupata majeraha ambayo yalimlazimu kwenda kufanyiwa matibabu ya kina.
Issa Liponda,Dar es Salaam