The House of Favourite Newspapers

Taifa Stars: Tuna Nafasi ya Kufuzu Kombe la Dunia

0

WAKATI Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars ikijiandaa na mchezo wa kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya DR Congo, meneja wa timu hiyo, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ amefunguka kuwa wana nafasi kubwa ya kufuzu michuano hiyo.

Stars ambayo ipo Kundi J, tayari imekusanya pointi saba ikiwa kileleni sawa na Benin, ikifuatiwa na DR Congo, kisha Madagascar.

 

Timu hiyo inayonolewa na Kocha Mkuu, Kim Poulsen, inajiandaa na mchezo dhidi ya DR Congo utakaopigwa Novemba 11, mwaka huu kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar, kisha Novemba 14, itakuwa ugenini kucheza na Madagascar.

Akizungumza na Spoti Xtra, Cannavaro alisema: “Timu inaendelea na mazoezi kuelekea mchezo wetu dhidi ya DR Congo.

 

“Wachezaji wanaocheza kwenye ligi za ndani wamewasili wote na hakuna majeruhi kwenye kikosi.

“Wengine wanaocheza soka nje ya Tanzania akiwemo Novatus Dismas tunatarajia atawasili leo (jana Jumamosi), wakati Simon Msuva na Mbwana Samatta tutawapokea Jumatatu.

 

“Tuna nafasi kubwa ya kufuzu maana vijana tutawapa morali na kuwaelewesha ili waweze kufanya vizuri kwa sababu ushindi dhidi ya DR Congo utatufanya tukae kwenye ile njia ambayo tunaitaka kwa muda mrefu sana.

 

“Tumefurahi sana kuwepo kwa mashabiki ambao ni elfu 30 katika mchezo huu, unajua shabiki ni mchezaji wa 12 uwanjani, hivyo tunawaomba Watanzania wajitokeze kwa wingi kwa ajili ya kutoa sapoti.”

LEEN ESSAU NA IBRAHIM MUSA, Dar

Leave A Reply