The House of Favourite Newspapers

Takwimu za Oktoba Zaibeba Yanga Dhidi Ya Simba

0
Niyonzima na Kamusoko.

HOMA ya mchezo wa Ligi Kuu Bara utakaozikutanisha Simba na Yanga katika ligi hiyo kwa mara ya kwanza msimu huu, tayari imeanza kupamba moto.

Timu hizo zitapambana Oktoba 28, mwaka huu katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam, mara ya mwisho kukutana uwanjani hapo ilikuwa ni Aprili 27, 2008 na matokeo yalikuwa ni suluhu.

Viongozi wa ufundi ya timu hizo, tayari wameshaanza kuweka mikakati yao sawa kwa ajili ya mechi hiyo ambayo mara nyingi huwaweka kwenye wakati mgumu wakihofia kupoteza ajira zao.

Ni rekodi nzuri ya Yanga iliyonayo kwa mechi zote ligi kuu ilizokutana na Simba mwezi Oktoba kuanzia mwaka 1965 ilipoanzishwa michuano hiyo.

Kwa upande wa Omog ni rekodi ya Simba iliyonayo katika Uwanja wa Uhuru kila inapokutana na Yanga, mwezi Oktoba.

Gazeti hili limechambua rekodi za mechi za ligi kuu baina ya timu hizo za mwezi Oktoba tangu kuanzishwa kwa ligi hiyo mwaka 1965.

Tangu mwaka 1965, Simba na Yanga zimekutana mwezi Oktoba mara 20, huku mechi saba kati ya hizo zikichezwa katika Uwanja wa Uhuru.

Katika mechi hizo 20 za mwezi Oktoba, Yanga imefanikiwa kushinda mechi saba na Simba imeshinda mechi sita huku zikitoka sare mara saba.

Katika mechi saba ambazo timu hizo zimekutana mwezi Oktoba kwenye Uwanja wa Uhuru, Simba imefanikiwa kuifunga Yanga mara nne huku Yanga ikiifunga Simba mara tatu.

Yanga ndiyo inayoongoza kwa kuzifumania nyavu za Simba mwezi Oktoba mara nyingi zaidi, imefanikiwa kuifunga mabao 19 katika mechi hizo wakati Simba yenyewe imefunga mabao 18.

Wachezaji wa Yanga ndiyo wanaoongoza kwa kuzifumania nyavu za Simba ndani ya mwezi huo.

Wachezaji wa Yanga wanaoshikilia rekodi hiyo ni Mohammed Hussein ‘Mmachinga’, Davis Mwape, Jerry Tegete na Hamisi Kiiza ambao kila mmoja ana mabao mawili aliyoyafunga katika mechi tofauti alizoitumikia timu hiyo ndani ya mwezi Oktoba.

Upande wa Simba, anayeshika rekodi hiyo kufunga mabao mengi katika mechi ilizozikutanisha timu hizo ndani ya mwezi Oktoba ni Nico Njohole ambaye pia ana mabao mawili.

 Sweetbert Lukonge, Dar es Salaam.

Leave A Reply