The House of Favourite Newspapers

Tambwe Aondolewa Kikosini Yanga SC

Amissi Tambwe

MSHAMBULIAJI wa Yanga, Mrundi, Amissi Tambwe, licha ya kupata nafuu ya majeraha yake ya goti, ameondolewa katika kikosi cha timu yake na kutakiwa kufanya mazoezi mepesi ya binafsi.

 

Tambwe, raia wa Burundi, ameongezewa wiki moja ya kuhakikisha hali yake inaimarika zaidi wakati timu yake leo ikicheza na St Louis ya Shelisheli kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

Daktari wa Yanga, Edward Bavu ameliambia Championi Jumamosi kuwa, Tambwe ameongezewa siku hizo baada ya kulalamikia maumivu wakati akifanya mazoezi magumu juzi.

 

Bavu alisema baada ya kumfanyia vipimo na kuonekana bado hayupo fiti, amemuongezea muda wa kukaa nje ya uwanja na kufanya mazoezi mepesi ya binafsi.

“Tunataka Tambwe akirejea uwanjani awe fiti kwa asilimia kubwa na hiyo ni baada ya hivi karibuni kulalamikia kusikia maumivu wakati anafanya mazoezi na wenzake.

 

“Ninaamini baada ya wiki moja atarejea uwanjani kwani hivi sasa anapata matibabu huku akiendelea na mazoezi binafsi kwa ajili ya kuwa fiti na kurejea uwanjani haraka,” alisema Bavu.

 

Wakati huohuo, Bavu alisema beki wa kati wa Yanga, Andrew Vincent ‘Dante’, ameanza kupata nafuu ya kufanya mazoezi ya ufukweni baada ya kusumbuliwa na maumivu ya misuli.

Comments are closed.