The House of Favourite Newspapers

Tambwe, Ngoma Warejea Kuwavaa Azam

 


Wilbert Molandi |CHAMPIONI| Dar es Salaam

WASHAMBULIAJI tegemeo wa Yanga, Mzimbabwe, Donald Ngoma na Mrundi, Amissi Tambwe, wamepata nafuu ya majeraha yao na leo Jumatatu watarejea rasmi uwanjani kujifua kwa ajili ya mechi dhidi ya Azam FC, Jumamosi ijayo.

Timu hizo, zinatarajiwa kuvaana Aprili Mosi, mwaka huu kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara uliopangwa kuchezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Wachezaji hao wanarejea mazoezini baada ya kukaa nje ya uwanja kwa muda wa wiki moja na nusu wakiuguza majeraha ya goti yaliyosababisha kuukosa mchezo wa marudiano wa Ligi ya Mabingwa dhidi ya Zanaco uliopigwa Lusaka, Zambia ambao ulimalizika kwa suluhu huku ikielezwa kuwa kama wangekuwepo basi Yanga ingeweza kupata bao ugenini na kuendelea mbele katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Daktari Mkuu wa timu hiyo, Edward Bavu alisema wachezaji hao wataanza kwa kufanya mazoezi ya binafsi kwa kukimbia mbio fupi na ndefu pamoja na yale ya viungo kwa hofu ya kujitonesha kabla ya kuanza ya pamoja na wachezaji wenzao.

Aliongeza kuwa, programu hiyo wataifanya kwa siku mbili kabla ya kufanya na wenzao na kikubwa wanatakiwa kuwepo kwenye mchezo dhidi ya Azam.

“Ni habari njema kwa mashabiki wa Yanga kuwa washambuliaji wao vipenzi, Ngoma na Tambwe kesho (leo) jioni wataanza mazoezi ya pamoja na wenzao,” alisema Bavu.

Comments are closed.