The House of Favourite Newspapers

Tambwe: Simu Moja Tu ya GSM, Mambo Fresh

0

STRAIKA wa zamani wa Yanga, raia wa Burundi, Amissi Twembe amefunguka kuwa Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Eng Hersi Said, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uwekezaji wa Kampuni ya GSM ambao ni wadhamini wa klabu hiyo wamempigia simu.

 

Tambwe aliyekuwa mkali wa kufunga mabao kwa kichwa ameeleza kuwa Injinia amemuomba amwambie mwanasheria wake apeleke hesabu za madai yake ili wamlipe.

 

Tambwe alifungashiwa virango na Yanga, mwanzoni mwa msimu uliopita, huku akidai fedha zake za mishahara na malimbikizo mengine zaidi ya shilingi milioni 41, akiwa sambamba na nyota wengine wa timu hiyo, kama Haji Mwinyi, Pato Ngonyani, Haruna Moshi ‘Boban’, Klaus Kindoki na wengine wengi, baada ya uongozi wa timu hiyo kudai kutengeneza timu, ambapo nafasi yake walimsajili David Molinga na Gnamien Yikpe.

 

Akizungumza na Championi Ijumaa, Tambwe alisema, ni kweli amepigiwa simu na Eng Hersi akimtaka amwambie mwanasheria wake, apeleke hesabu kamili anazoidai Yanga ili wazilipe mapema iwezekanavyo, kwani wao hawakuwa na nia mbaya ya kutotaka kumlipa zaidi hawakuwa wanajua sahihi idadi ya madai yake.

 

“Nashukuru Mungu Yanga kupitia kwa mdhamini wao GSM, amenipigia simu jana (Jumatano) tuliongea akasema mwanasheria wangu nimwambie afanye hesabu ya hela yote ninayowadai ili na wao waweze kufanya malipo kama ambavyo Fifa imewataka.“

 

Kimsingi watu hasa mashabiki wa mpira wa Tanzania wakiwemo Yanga, hawatakiwi kunilaumu mimi zaidi wanapaswa kujua kuwa, mimi na Yanga, hatujauziana kitu jamani, ila mimi nadai changu ambacho nilitoleaga jasho tu,” alisema Tambwe.

 

Pamoja na Tambwe kueleza hivyo, Jumatano iliyopita, Eng Hersi alikaririwa akisema hivi: “Usajili Yanga utaendelea kama kawaida na haitafika Ijumaa (leo) hiyo milioni 41 tutakuwa tumeshailipa, hatukuwepo mapema tu sisi GSM kwenye ishu hii.

 

“Ninachotaka kuwahakikishia wanachama na mashabiki wote Yanga, GSM tupo imara kuijenga timu ndani ya uwanja na nje ya uwanja kwa kuwapa kilicho bora Wanayanga wote.”

MUSA MATEJA, Dar es Salaam

MOTO wa POLEPOLE BUNGENI LEO, ALIVYOSIMAMA KWA MARA YA KWANZA KUCHANGIA HOTUBA YA MAGUFULI…

Leave A Reply