The House of Favourite Newspapers

TANASHA ANAVYOTEKETEZA MAMILIONI YA MONDI

STAA wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ na mchumba wake kutoka nchini Kenya, Tanasha Donna ndiyo ‘kapo’ inayotikisa kwa sasa Afrika Mashariki ambapo kutokana na kila mmoja kuishi mbali na mwenzake tangu walipoanzisha uhusiano wao mwaka jana, wamekuwa wakilazimika kukutana kwa gharama kubwa.  Diamond au Mondi anaishi Dar wakati Tanasha anakaa jijini Mombasa, Kenya anakofanya kazi ya utangazaji katika Kituo cha Redio cha NRG. Tanasha, katika moja ya mahojiano jijini humo hivi karibuni aliweka wazi kuwa amekuwa akisafiri kwa ndege mara kwa mara kwa ajili ya kumfuata mpenzi wake Mondi jijini Dar ili kuoneshana mahaba huku mkwanja ukidaiwa kutolewa na jamaa huyo ambaye ni Prezidaa wa Wasafi Classic Baby (WCB).

Tanasha alitoa jibu hilo baada ya kuulizwa kwamba anawezaje kumudu kuwa na mpenzi nchi nyingine na maisha ya furaha yakaendelea kuwepo na jibu lake lilikuwa hivi: “Umbali siyo tatizo na halijawahi kuwa tatizo kwa sababu popote alipo ninaweza kuchukua usafiri wa ndege nikamfuata kila wikiendi na tukawa wote bila tatizo. Kutoka Nairobi ni kama saa moja tu hivi kumfikia na suala la gharama siyo ishu.”

Lakini safari hizo za Tanasha kwenda Tanzania kila wikiendi zina maana gani kwa Mondi? Maana yake ni kwamba, pesa ya kumsafirisha mpenzi wake huyo ipo na kwamba kinachotakiwa ni kukutana kila wakati ili kudumisha penzi bila kujali gharama!

Hata hivyo, staa huyo wa Wimbo wa Inama anaweza kufanya hivyo kwa kuwa bado muziki wake unafanya vizuri hata  kama kwa sasa amesimama kufanya shoo kupisha Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, lakini wengi wanaamini mwanadada huyo anatumia vilivyo pesa za Mondi.

Uchunguzi umebaini kwamba, jamaa huyo amekuwa akitumia pesa ndefu kwa ajili ya kugharamia safari za Tanasha achilia mbali shopping za hapa na pale pamoja na matumizi mengine mwanadada huyo awapo Bongo. Mpaka sasa Tanasha na Mondi wamekuwa pamoja kwa zaidi ya miezi sita, hii ni sawa na wikiendi 24 ambazo zote Tanasha alisafiri kumfuata Mondi.

Kwa sasa gharama za ndege za kwenda na kurudi kutoka Nairobi hadi Dar kwa kutumia ndege za Shirika la Ndege la Kenya Airways ni kama shilingi 34,800 za Kenya (zaidi ya shilingi 800,000 za Kibongo). Hii ni kwenda na kurudi kwa wikiendi moja. Maana yake ni kwamba, Mondi (kama ndiye anayehusika na gharama zote) ametumia kiasi cha shilingi 835,200 za Kenya (zaidi ya milioni 18) kwa ajili ya Tanasha kukatia tiketi za ndege pekee kwa wikiendi 24 zilizopita.

“Yule mtoto (Tanasha) atakuwa anateketeza pesa kibao za Diamond, hizi safari za kila mara kuja Dar na kurudi Nairobi ukijumlisha na matumizi mengine kwa mwezi inakatika pesa si ya kitoto, hii yote inaonesha wanapendana na pesa siyo ishu katika kuboresha uhusiano wao,” aliandika mdau mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Sued baada ya kuona picha ya Mondi na Tanasha kwenye mtandao wa Instagram.

Uhusiano huu wa Mondi na Tanasha ni tofauti kabisa na ilivyokuwa kwa Mondi na Zari ambaye hakuwa anafanya safari nyingi za Dar kama anavyofanya Tanasha. Zari na Mondi walikuwa wakionana mara chache mno walipohitajiana, jambo ambalo Mondi aliwahi kukiri kuwa ndiyo chanzo cha kuchepuka na mwanamitindo Hamisa Mobeto

Comments are closed.