Ticha mjamzito achomokea dirishani kwenye daladala
CHEZEA kifo wewe! Mwalimu wa Shule ya Msingi Mwere ya mjini hapa ambaye jina halikupatikana mara moja, akiwa mjamzito, amenusurika kifo baada ya daladala walilopanda kutumbukia mtaroni na yeye kuchomokea kwenye dirishani.
Tukio hilo lilijiri jirani kabisa na eneo la Kanisa la KKKT ambapo mashuhuda walidai kwamba tukio hilo lilitokea baada ya dereva wa daladala aliyefahamika kwa jina moja la Mathias kumuachia ‘deiwaka’ kijana mwingine aliyetajwa kwa jina la Arird Tito.
Shuhuda huyo aliendelea kusimulia kwamba, Arird hakuwa dereva mwenye ujuzi hali iliyomfanya kutojua sheria za usalama barabarani hivyo akalazimisha kulipita gari kubwa lililokuwa mbele yake kwa kutumia upande wa kushoto badala ya ule uliozoeleka wa kulia.
Baada ya dereva wa gari kubwa kuona hivyo hakumpa nafasi dereva huyo ndipo akajikuta anatumbukia mtaroni.
“Baada ya gari kutumbukia mtaroni, ticha huyo na madenti wake walilazimika kuokoa maisha yao kwa kutokea kwenye madirisha ya daladala hiyo,’’ alisema Tito ambaye alikuwa ni kondakta wa daladala hiyo.
Hata hivyo, abiria hao hawakuumia sana zaidi ya kupata michubuko ya hapa na pale, kabla ya kupelekwa hospitalini kwa matibabu.