TID alala selo siku 3
Mkali wa voko kunako Bongo Fleva, Khaleed Mohamed ‘TID Mnyama’.
Musa mateja
Mnyama Unyamani! Mkali wa voko kunako Bongo Fleva, Khaleed Mohamed ‘TID Mnyama’, amejikuta akilala selo yapata siku tatu, ni Ijumaa Wikienda pekee lenye ubavu wa kuandika.
Habari kutoka kwa chanzo makini ndani ya polisi zilieleza kuwa, TID alikutwa na msala huo wikiendi iliyopita kufuatia kumpa kipondo ‘hevi’ kijana mmoja waliyevurugana naye kisha kushtakiwa kwenye Kituo cha Polisi cha Oysterbay, Kinondoni jijini Dar.
Ilifahamika kwamba, mara ya kwanza aliswekwa ndani na baadaye akatolewa kwa sharti la kumtaka amlipe kijana huyo kiasi cha Sh. milioni tatu, jambo ambalo TID hakulitekeleza hivyo kukamatwa tena na kulala selo kwa siku tatu.
Baada ya kumwagiwa ‘ubuyu’ huo, gazeti hili liliingia mzigoni kupata undani wa sakata hilo ambapo lilizama Kituo cha Polisi Oysterbay alikokuwa ameshikiliwa staa huyo wa Ngoma ya Kiuno.
Habari zilizopatikana zilithibitisha kushikiliwa kwa TID kabla ya kuachiwa juzi usiku baada ya kumalizana na jamaa huyo.
Hata hivyo, usiku huohuo, TID alinaswa kwenye ‘bethedei’ ya Mwanamuziki Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ iliyofanyika nyumbani kwake, Madale-Tegeta, Dar ambapo alifanya mazungumzo na gazeti hili juu ya ishu hiyo.
“Nashindwa kuelezea maana nipo hapa kwa ajili ya kufurahi na si kukumbuka machungu ila kweli kuna kijana tulitibuana, akanipeleka polisi ila tumekwishamalizana,” alisema TID.