The House of Favourite Newspapers

Tigo Yachangia Simu 1,350 Upatikanaji Wa Vyeti Vya Kuzaliwa

0

Tigo Tanzania inayo furaha kwa mara nyingine tena kuendelea kushirikiana na serikali kupitia taasisi ya RITA na wadau wengine ikiwemo UNICEF, VSO katika awamu ya tano ya Mkakati wa Usajili wa watoto chini ya miaka mitano kwa mikoa ya Kilimanjaro na Tanga.

Kampuni ya Tigo imekuwa mstari wa mbele katika kuendeleza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika sekta mbalimbali ikiwemo ya ustawi wa jamii ambapo tumefanikiwa kuonyesha umuhimu wa matumizi ya teknolojia ya simu za mkononi kama nyenzo muhimu katika kufikia malengo endelevu na mradi huu ni mfano halisi.

Sote tunatambua umuhimu wa utambulisho (identity) na takwimu katika kurahisisha upatikanaji wa huduma za kijamii k.m afya, elimu na kadhalika.

Waziri wa Katiba na Sheria Dkt Mwigulu Nchemba akisalimiana na Daniel Mainoya- Meneja wa Tigo, kanda ya kaskazini alipotembelea maonesho ya Nane Nane mkoani Arusha .

Hata katika usajili wa laini za simu tunahitaji utambulisho stahiki ambao chanzo chake ni cheti cha kuzaliwa. Hivyo basi umuhimu wa watoto wetu kusajiliwa na kupata vyeti pindi wanapozaliwa ni jambo linalohitaji kupewa kipaumbele cha juu zaidi na wadau wote.

Tigo tumeendelea kuwekeza katika mradi huu wa usajili wa watoto chini ya miaka mitano toka tulivyozindua mkoa wa kwanza yaani Mbeya na umekuwa tukichangia simu za mkononi zinazotumika katika Usajili kwa mikoa yote 16,ambapo mpaka sasa wamesajiliwa Watoto zaidi ya million 4.3. Na kwa Kilimanjaro na Tanga tunachangia simu za mkononi (smart phones) 1,350 zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 168,750,000. Simu hizi ndizo watakazotumia wasajili waliopatiwa mafunzo ili kuhakikisha watoto wa Kilimanjaro na Tanga wanasajiliwa taarifa zao zinatumwa kupitia mfumo wa SMS kwenda RITA.

Waziri wa Katiba na Sheria Dkt Mwigulu Nchemba akipata maelezo kutoka kwa Afisa wa Tigo Kuhusu Huduma mbali mbali zinazotolewa katika Banda la Tigo. alipotembelea maonesho ya Nane Nane mkoani Arusha

Tigo inatambua ukweli kwamba Cheti cha kuzaliwa ni nyaraka ya awali ya utambulisho kwa mtoto inayomwezesha kutambuliwa uwepo wake na ni haki yake ya msingi. Hivyo, tunahamasisha wazazi na walezi kuchangamkia fursa hii na kuhakikisha watoto wote wamesajili na kupatiwa vyeti.

Kwa mara nyingine tena tunapenda kuwashukuru wadau wetu wote kwa kuendelea kushirikiana nasi na vile vile tunapenda kuhakikishia serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na wadau wote wa maendeleo kuwa tutaendelea kushiriki katika miradi mbalimbali yenye kuleta tija na hasa inayolenga kuendeleza matumizi ya TEHAMA kwa ustawi jamii na uchumi.

Leave A Reply