The House of Favourite Newspapers

Tshishimbi Atua Pemba, Yanga Kamili Gado

0
Kiungo mkabaji ametua Yanga, Papy Kabamba Tshishimbi (kushoto) akifanya yake.

MZIKI wa Yanga sasa upo kamili gado kwani kiungo mkabaji Papy Kabamba Tshishimbi ametua jijini Dar es Salaam kisha jana akajiunga na wenzake kambini kisiwani Pemba kujiandaa na mechi dhidi ya Simba.

Yanga imeweka kambi yake Pemba kujiandaa na mechi hiyo dhidi ya Simba ambayo ni ya Ngao ya Jamii itakayochezwa Agosti 23, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Awali, Tshishimbi raia wa DR Congo, alisaini mkataba lakini akashindwa kujiunga na wenzake akielezwa kurudi nchini kwao kumaliza baadhi ya taratibu zake za uhamiaji.

 

Tshishimbi alitua jijini Dar es Salaam, juzi na jana jioni akapandishwa ndege na viongozi wa timu hiyo kuelekea Pemba kujiunga na wenzake.

 

Awali kulikuwepo na sintofahamu ya wapi aliko kiungo huyo lakini, baadaye Yanga ikafafanua kila kitu kuhusu Tshishimbi kwamba alirudi kwao kuweka mambo sawa na juzi akatua nchini.

 

Mmoja wa maofisa wa Yanga alilithibitishia Championi Jumamosi, jana kwamba, Tshishimbi aliyesaini mkataba wa miaka miwili kutoka Mbabane Swallows ya Swaziland, ametua nchini na tayari ameenda Pemba.

 

“Tshishimbi amewasili nchini tayari tangu jana (juzi) na leo (jana) ameenda Pemba kujiunga na wenzake tayari kwa kambi ya kujiandaa na mechi dhidi ya Simba.

 

“Tunategemea atakiongezea nguvu kikosi chetu kuelekea mchezo wetu na Simba ambao tutacheza Jumatano ya wiki ijayo, hii ni habari njema kwetu,” alisema bosi huyo.

 

Habari kutoka Pemba zimesema, Tshishimbi alitua kwenye Uwanja wa Ndege wa Pemba saa 9:45 alasiri na kupokelewa na Meneja wa Yanga, Hafidh Saleh.

 

Mmoja wa watu wa benchi la ufundi wa Yanga alisema, kutua kwa kiungo huyo Pemba kutashusha presha ya Kocha wa Yanga, George Lwandamina katika kuelekea mchezo dhidi ya Simba.

“Tumeshampokea Tshishimbi hapa Pemba na moja kwa moja ataanza mazoezi ya pamoja na wenzake kwa ajili ya kujiandaa na mechi ya Ngao ya Jamii dhidi ya Simba,” alisema mtoa taarifa wetu kutoka Pemba.

 

Alipotafutwa meneja Saleh kuzungumzia hilo alisema; “Ni kweli nimetoka kumpokea Tshishimbi muda huu (jana) Uwanja wa Ndege wa Pemba na moja kwa moja akajiunga na kambi ya pamoja.

 

“Amejiunga na timu akitokea kwao Kongo alipokwenda kukamilisha baadhi ya vitu ikiwemo pasipoti yake ambayo ilikuwa imeisha, hivyo alitakiwa kuikamilisha ndiyo ajiunge na timu.

“Na mara baada ya kujiunga na timu leo (jana) jioni anatarajiwa kujiunga na wachezaji wenzake kwa ajili ya mazoezi ya pamoja kujiandaa na mechi ya Simba.”

 

Wakati huohuo, Yanga kesho Jumapili itacheza mechi ya kirafiki na Jamhuri ya Pemba kwenye Uwanja wa Gombani uliopo Pemba. Pia kipa Ramadhan Kabwili amepumzishwa kwa saa 24 ili kutuliza mwili wake kutokana na uchovu.

Stori: Wilbert Molandi na Musa Mateja | Championi Jumamosi

VIDEO: Vilio Tena Shule ya Lucky Vincent, Arusha (VIDEO)


Leave A Reply