SHIRIKA la Mawasiliano Tanzania (TTCL) leo limezindua duka jipya na kituo cha huduma Kariakoo eneo la Mtaa wa Mafia na Msimbazi jijini Dar es Salaam ikiwa ni jitihada za kusogeza huduma zake karibu zaidi na wateja.
Akizungumza katika uzinduzi huo Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Mawasiliano Tanzania ( TTCL), Mhandisi Omary Nundu alisema kwa Mwaka 2019, TTCL imejipanga vyema kuhakikisha kuwa Huduma za Shirika hilo zinasambaa zaidi kote nchini huku ikisimamia ubora na unafuu wa gharama ambazo zitakuwa nafuu kwa wananchi.
“…Tunakusudia kuendelea kufanya mageuzi makubwa ndani ya Shirika ili kuliwezesha kushindana kikamilifu katika Soko la Huduma za Mawasiliano Nchini sambamba na kutimiza wajibu wa kimsingi wa kuwa mchangiaji muhimu katika Pato la Taifa,” alisema Mhandisi Omary Nundu.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TTCL Corporation, Bw. Waziri Waziri Kindamba awali akizungumza alisema uzinduzi huo wa duka na kituo cha Huduma kwa Wateja ni utekelezaji wa Mpango Mkakati wa miaka mitatu, 2016-2019 ambao umeweka msisitizo mkubwa katika kuboresha eneo la Huduma kwa Wateja.
“Uzinduzi wa leo unaonesha kwa vitendo jinsi gani TTCL mpya ilivyojipanga vyema kuhakikisha huduma zake zinawafikia Wateja katika mazingira mazuri, yanayovutia na kuwakilisha hadhi ya Shirika letu. Kukamilika kwa Duka hili/ Kituo hiki cha Huduma kwa Wateja kuonaongeza idadi ya Maduka mapya ya TTCL kufikia maduka 10 ambayo yamejengwa kwa viwango vya hali ya juu na kwa kuzingatia mahitaji ya sasa ya utoaji bora wa Huduma kwa Wateja,”
Aidha aliongeza kuwa TTCL itaendelea kuboresha Maduka na Vituo vyote Nchi nzima, sambamba na Ofisi zake za Mikoani na Wilayani ili ziweze kuwa mahali bora kabisa kwa Watumishi wa TTCL wanaotoa huduma na wateja wote watakaofika kupata huduma za aina mbalimbali.
Comments are closed.