KWENYE wengi kuna mengi; usifikiri kila anayekwenda kwenye shoo za muziki anafuata burudani kuna wengine wana agenda zao kichwani. Njemba mmoja (jina halikupatikana) aliyezamia shoo ya Wasafi Festival iliyofanyia jijini Mwanza mwishoni mwa wiki iliyopita yalimkuta mazito baada ya kudaiwa kubadili gia ya shoo na kuanza kubambiabambia wanawake.
Sijui ndiyo alikumbwa na ule wanaouita mfadhaiko au uzalendo ulimsinda au jini mahaba; lakini ukweli ni kwamba baadhi ya akina dada waliokuwa karibu naye walidai alikuwa ‘akiwasumbua’ na hivyo kumpigia mayowe. “We kaka vipi, kwa nini unanipapasa,” alisikika akisema mwanamke mmoja huku akiungwa mkono na wengine wawili jambo lililozua vurugu katika eneo hilo.
Mara baada ya amani kutoweka wazee wa kutuliza watukutu kwenye shoo a.k.a mabaunsa walivamia eneo hilo na kumtoa bila adabu njemba huyo huku wakimtembezea kichapo. Ukiangalia picha ukurasa wa nyuma utaamini kuwa, jamaa huyo alijutia kosa alilolifanya kwa sababu mtu mzima kuangua kilio si jambo la kuigiza.
Kazi ya kumthibiti njemba huyo ilikamilishwa na mabaunsa kwa kuhakikisha kuwa ametoka nje ya Uwanja wa CCM Kirumba mlimokuwa mkifanyika shoo hiyo iliyokusanya wasanii kibao na kujaza umati. Miongoni mwa wasanii hao ni pamoja na Nasibu Abdul ‘Diamond’ na kruu nzima ya Wasafi Classic Baby ‘WCB’, Dudu Baya, Gigy Money na Mlkia wa Taarabu, Khadija Kopa (pichani juu).
STORI: MWANDISHI WETU, UWAZI
Comments are closed.