The House of Favourite Newspapers

TUKIO LA KUTISHA! Mtoto Miaka 8 Acharangwa Vibaya Mgongoni

MKURANGA: Duniani kuna mengi, ukiwa mzima mambo ya kuona na kusikia yapo ya kutosha; mfano ni hili tukio la kutisha lililompata mtoto wa miezi minane, mkazi wa Kijiji cha Kikurwi, Mkuranga mkoani Pwani.

 

Kutokana na maudhui jina na sura ya mtoto vinafichwa lakini mama yake mzazi aitwaye Asia Athumani, aliliambia Uwazi hivi karibuni kuwa, mwanaye huyo Jumanne iliyopita alikumbwa na mkasa wa kushangaza.

 

Ni mkasa gani huo? Asia anasimulia: “Nilikuwa ndani nyumbani kwangu napika, ghafla nikasikia mwanangu aliyekuwa nje akicheza analia. “Nikaamua kutoka ili kuona kinachomliza, nikashangaa kukuta amezingirwa na kundi la nyani waliokuwa wakimvuta na kutaka kuondoka naye.”

 

Heeh! Nyani wamvute mtoto na kutaka kuondoka naye, waende naye wapi wakati wao chakula chao siyo nyama?

Hakika lilikuwa si tukio la kawaida ambapo mama huyo anaeleza kuwa, baada ya kuona hivyo alianza kupiga kelele kuomba msaada wa majirani waje wamnusuru mwanaye. Alieleza kuwa, wakati akiomba msaada huo naye alikuwa akipambana kuwakabili nyani hao ambao wakati huo walikuwa wakivutana huku kila mmoja akitaka aondoke na mtoto huyo.

 

Katika purukushani nyani hao walijikuta wakimjeruhi vibaya mtoto huyo sehemu mbalimbali za mwili wake hasa mgongoni kutokana na mikono ya wanyama hao kuwa na kucha ndefu. Hata hivyo, Mungu alisadia nyani hao walipoona watu wameanza kujitokeza, walimtelekeza mtoto huyo na kutokomea zao kwenye vichaka vinavyozunguka makazi ya watu katika kijiji hicho. Kufuatia tukio hilo mtoto huyo alikimbizwa Hospitali ya Wilaya ya Mkuranga ambako alipatiwa matibabu.

Mama wa mtoto huyo aliliambia Uwazi kuwa pamoja na mwanaye kupatiwa matibabu na hali yake kuendelea vyema, bado anakabiliwa na uhaba wa fedha za kununulia dawa. “Kuna dawa niliandikiwa ambazo zina gharama kama ya shilingi 100,000, madaktari wameniambia kuwa dawa hizi zinapatikana Dar es Salaam,” alisema Asia.

 

Katika hatua nyingine, mama huyo alimshukuru Mungu kwa kumwezesha mwanaye kuokolewa vinginevyo nyani hao wangeweza kumuua. Naye mama mkubwa wa mtoto huyo aliyejitambulisha kwa jina la Asha Athumani, alisema nyani katika kijiji chao wamekuwa tishio kubwa na hasa kwa wanawake ambao alisema kuwa kwa tabia ya wanyama hao huwaogopa zaidi wanaume.

 

“Yaani hawa nyani ni kama watu kuna kipindi unaona kabisa kama wanafanya mambo kwa visirani na ole wako mtoto wao labda aharibu mazao yako halafu umpige. “Watakushambulia mpaka utapiga mayowe ya kuomba msaada na bora kidogo wanaume huwa wanawakimbia lakini wanawake wanatudharau sana,” alisema Asia.

 

Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya Mkuranga, Steven Mwandambo alithibitisha kumpokea mtoto huyo ambaye anaendelea kutibiwa hospitalini hapo na kusema hali yake inaendelea vizuri. “Alivyoletwa alikuwa na hali mbali kutokana na majeraha hayo, lakini mpaka sasa anaendelea vizuri,” alisema Dk. Mwandambo.

NYANI NI VIUMBE GANI?

Kifupi nyani ni wanyama wanaofanana na sokwe. Wana ukubwa unaokaribiana na mbwa na wengine wamezidi kidogo na hasa madume. Mara nyingi hupenda kutembea kwa makundi. Chakula chao kikuu ni nafaka na hasa mahindi mabichi. Wanakula pia maboga, maembe, mihogo, uyoga na mimea mwitu mbalimbali. Mara nyingi historia imekuwa ikijaribu kuwalinganisha wanyama hao na binadamu kutokana na jinsi tabia zao zinavyofanana na binadamu.

 

Ni wanyama wanaotajwa kuwa na uelewa mkubwa ukilinganisha na wanyama wengine kama swala na twiga. Huweza kuwachagua chawa watoto wao na kuwalinda wakati wa mvua na hatari nyinginezo. Lakini sokwe ambao ni aina pia ya nyani ila wenyewe ni wakubwa zaidi, wanatajwa kuwa na ufahamu mkubwa kuliko wa nyani.

JIUNGE NA FAMILIA YA GLOBAL TV UPANDE MTANDAO WA MAFANIKIO

KARIBU ujiunge na familia ya marafiki wa Global TV Online – Club sasa, uwe wa kwanza kupata video zote za Global TV, video za hamasa kutoka kwa Eric Shigongo, breaking news za matukio yote duniani, michezo na dondoo za afya. Utapata nafasi ya kuingia bure na kutazama shoo, matamasha, semina na burudani zinazoandaliwa na Global TV mikoa yote Tanzania.
Pia, ukiwa na tatizo la kifamilia mfano misiba, kuuguliwa na majanga, marafiki zako wa Global TV Club tutakusaidia.
 
Pia, tutakuunganisha na mtandao wa marafiki zetu waliyofanikiwa ndani na nje ya Tanzania, ili upate mafunzo maalum ya kujikwamua kutoka katika hali duni ya maisha.

Bofya hapa kujiunga na familia ya Global TV Club ==> Global TV Family Club

Comments are closed.