The House of Favourite Newspapers

Tume ya Haki za Binadamu Inachunguza Haki za Binadamu na Utawala Bora Viwanda vya Pwani

Kutoka kushoto ni Meneja wa Keds, Michael Baraka Lugalela, Mkurugenzi wa Kiwanda hicho, Bob Chen na Afisa Habari wa Kiwanda Ali Yusuph Nasir wakizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo pichani).
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imeanza ziara ya wiki mbili wakifanya uchunguzi wa kero na malalamiko ya wafanyakazi na wakazi wa maeneo jirani ya viwanda vya mkoa wa Pwani.
Akizungumza  na Waandishi wa Habari leo tarehe 12 Machi 2025 Kamishna wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) Nyanda  Shuli katika ziara hiyo wilayani Kibaha amesema
lengo la ziara hiyo ni kuangalia hali ya haki za binadamu na uzingatiwaji wa misingi ya utawala bora usalama wa mazingira ya kazi na uzingatiwaji wa viwango vya ajira kiwandani  hapo.
Kamishna  amesema kuwa wamefika hapo na kujionea hali halisi na kusisitiza tume itafanya uchunguzi wake  kwa kutumia wakaguzi wao, kadhalika OSHA watakuja tena kufanya ukaguzi  pia tayari walishakuja katika siku za nyuma kulikua na changamoto walizozibaini lakini  tayari uongozi  umeshazirekebisha  baadhi ya changamoto hizo.
“Tume ni sawa na sikio la Serikali pindi tunapopata malalamiko  kutoka kwa wananchi tunanyanyuka  ofisini  na kwenda kuwatembelea ikiwa ni pamoja  na kuongea  na pande zote mbili,hadi Tume kufika hapa ieleweke kuwa kuna kitu kimetuleta”
“niseme tu nawashukuru wananchi kwa kutoa taarifa ukiona haki yako inavunjwa au ukaona haki ya mtu mwingine inavunjwa na ukakaa kimya  jua kuna siku haki yako  itavyunjwa” amesema Kamishna  Shuli.
Akifafanua  kuhusu muda sahihi  wa kutatua malalamiko  waliyoyapata amesema kuwa  kadri  uchunguzi unavyoendelea  kuna mambo yatajitokeza, mfano hayo maji yanayolalamikiwa na wananchi kwamba  yanatiririshwa kutoka Kiwandani itakazimu wataalamu waje wayachukue wakayapime kama kwani wao ndiyo wenye mamlaka ya kutoa majibu sahihi amesema Kamishna.
Aidha amesema kuwa Tume hiyo itaendelea na ziara ya kutembelea viwanda  ambavyo wananchi wametoa malalamiko.
Aidha Kamishna  ametoa shukrani  kwa Uongozi  wa Kiwanda Cha Keds  kwa ushirikiano  mkubwa  waliowaonesha.
“Tume imeambatana  na Taasisi za Serikali ambazo ni OSHA, NEMC na Maafisa kutoka Ofisi ya RAS ,Afisa Biashara, Afisa Kazi na Afisa Maendeleo ya jamii wote kutoka Mkoa wa Pwani huku lengo kubwa  likiwa kuleta ufanisi katika ziara hiyo.
Naye Mkurugenzi Mtendaji  wa Kiwanda cha Keds Bob Chen amesema kuwa Kiwanda chao ni wazalishaji wa  bidhaa za sabuni, taulo za kike na taulo za kike ambazo huuzwa ndani ya nchi na nje ya nchi huku wakizingatia sana usalama wa afya za wafanyakazi pamoja na jamii inayoishi katika maeneo ya  jirani ya kiwanda hicho.
“Asilimia 60 ya wafanyakazi wetu wanaishi jirani  na Kiwanda hivyo kama kungekua na madhara basi wangeanza kudhurika wao hata kwenye rekodi zetu hatujawahi kupata malalamiko  ya namna yoyote”
amesema Bob.
Amekanusha kwamba  maji yanayotiririka kutoka Kiwandani hapo kuwa hayana sumu kwani malighafi kuu ni mchanga na laiti kama yangekuwa na sumu basi wafanyakazi wao ambao wanashinda na kukesha kiwandani wangeshapata madhara.
Meneja wa Keds Tanzania Limited Michael Lugalela amesema kuwa kiwanda hicho kimejengwa kwa dhamira njema na lengo kubwa kukuza uchumi wa nchi na mwananchi mmoja mmoja ikiwa ni pamoja na kutoa ajira  kwa mkoa  na kukuza uchumi wa nchi kwa ujumla.