The House of Favourite Newspapers

UBUYU! CHAZ BABA ABADILI DINI ILI AOE MKE MWINGINE

UBUYU siku nyingine lazima uchanganywe na pilipili kidogo ili uweze kuleta ladha ya tofauti kabisa!

Ubuyu wa leo ni wa mwanamuziki wa Dansi Bongo anayeitumikia Bendi ya The African Stars ‘Twanga Pepeta’, Charles Gabriel ‘Chaz Baba’.

Chaz Baba anadaiwa kubadilisha dini kutoka Ukristo kwenda Uislam ili aweze kuoa mke mwingine huku ndoa yake ya kwanza na mwanamama Rehema Sospeter ambaye alifunga naye kanisani ikidaiwa kuvunjika.

 

TUJIUNGE NA MLETA UBUYU

Kwa mujibu wa mleta ubuyu wetu, kulikuwa na mgogoro wa mda mrefu kati ya Chaz Baba na mkewe huyo kiasi ambacho kuna kipindi mkewe huyo alikuwa akiondoka na kurudi kwao kisha kurejea tena kwa mumewe.

Ilisemekana kwamba ilikuwa ni kawaida yao kutofautiana na kuyamaliza, lakini safari mkewe aliondoka na hakurudi tena.

 

Ilidaiwa kuwa, baada ya mkewe kugoma kurudi ndipo Chaz Baba akaanza harakati za kutaka kuoa kwa kubadili dini.

“Unajua sasa hivi Chaz Baba anataka kuoa mwanamke mwingine na tayari ameshabadilisha dini na jina kwa ajili ya kumuoa huyo mwanamke mpya baada ya mkewe kugoma kurudi kwake,” alisema mto ubuyu wetu huyo kwa sharti la kutotajwa gazetini.

 

HUYU HAPA CHAZ BABA

Baada ya kulambishwa ubuyu huo mtamu, Ijumaa Wikienda lilimtafuta Chaz Baba au Kingunge kuhusu ishu hiyo ambapo mambo yalikuwa hivi;

Ijumaa Wikienda: Mambo vipi Chaz Baba? Kuna habari kuwa umebadilisha dini na jina kwa ajili ya kuoa mwanamke mwingine wa Kiislam, je, huu ubuyu ukoje?

Chaz Baba: Ni kweli kabisa na sasa hivi ninaitwa Adulkarim na ndoa yangu ni mwezi ujao (mwezi wa kumi na moja).

NDOA YA KIKRISTO INAVUNJIKA?

Ijumaa Wikienda: Lakini najua ulifunga ndoa ya Kikristo kanisani ambayo ni ngumu kuvunjika, je, imekuwaje?

Chaz Baba: Hata ndoa ya kanisani inavunjika tu, kwa hiyo hata kama mwanamke amekuzingua uendelee naye? Sasa kwa taarifa yako kwangu imewezekana kuvunjika.

Ijumaa Wikienda: Na je, akija kwenye harusi kufanya fujo si ni haki yake?

Chaz Baba: Asithubutu kwani atapigwa kwa sababu aliondoka mwenyewe nyumbani wakati mimi nikiwa safarini.

 

ANAMUOA SAJENTI?

Ijumaa Wikienda: Mwanamke unayemuoa ni Sajenti (mwigizaji Husna Idd) maana umekuwa ukihusishwa naye na pia ni Muislam?

Chaz Baba: Sajenti? (kicheko) hapana, mke wangu mtarajiwa siyo maarufu hata kidogo. Yeye yupo bize na kazi zake tu maana ni mfanyabiashara.

 

Ijumaa Wikienda: Ni ngumu sana wanaume kubadili dini na tumezoea wanawake wakifanya hivyo, je, wewe ni nini kimekusukuma?

Chaz Baba: Mimi wala haikuwa ngumu, ni kwa sababu ninampenda na ninaona nay eye ananipenda sana.

Ijumaa Wikienda: Poa ninakushukuru sana Chaz Baba.

Chaz Baba: Asante sana.

 

MKEWE VIPI?

Ijumaa Wikienda lilifanya jitihada za kumpata mke wa Chaz Baba lakini ziligonga mwamba.

Kwa muda mrefu ndoa ya Chaz Baba imekuwa na vibwanga vingi huku madai yakishushwa kwamba jamaa huyo alikuwa na mkono mwepesi wa kumpiga mwenza wake huyo.

MAKALA: Imelda Mtema, DAR

Comments are closed.