The House of Favourite Newspapers

Ukatili! Mama wa Kambo Amchoma Kisu Mtoto

Mama mmoja mkoani Tanga aliyefahamika kwa jina moja la Ashura, amemchoka kwa kisu mtoto wake wa miaka nane kwa madai ya kuvunja chupa ya chai.

 

Mtoto huyo Zainabu Hussein (8), ambaye pia ni mwanafunzi wa darasa la pili katika Shule ya Msingi Changa iliyopo jijini Tanga, amesema kabla ya kuchomwa kisu kilichowekwa kwenye moto alichapwa viboko kwa sababu aliangusha chupa ya chai.

Mtoto huyo aliyekuwa akilia kwa uchungu muda wote kutokana na majeraha makubwa mwilini mwake ameomba msaada wa kupelekwa kwa mama yake aliyesema anaishi mkoani Dodoma.

 

“Siku ya Jumamosi mama Ashura alinichapa na kisha kunichoma na kisu ambacho alikuwa amekiweka kwenye moto kwa sababu nilikuwa nimebeba chupa ya chai kwa bahati mbaya ikaanguka na kupasuka ndiyo mama akanipiga halafu akachukua kisu na kukiweka kwenye moto kisha akaanza kunichoma nacho mwilini,” anaelezea Zainabu huku akilia kwa uchungu.

 

Kuhusu baba yake, mtoto huyo amesema baba yake anafanya kazi katika Kiwanda cha Saruji mkoani hapo, ambapo siku aliyopigwa na kuchomwa na kisu mama huyo baba yake alikuwa kazini na alirudi usiku hakuweza kuonana naye hivyo baba huyo hatambui suala hilo.

Licha ya kubembelezwa na watu mtoto huyo alikuwa akilia huku akisisitiza apelekwe kwa mama yake anayeishi Majengo jijini Dodoma.

 

Aidha, Mtanzania Digital pia ilizungumza na mama Ashura kufahamu chanzo cha adhabu hiyo kubwa kwa mtoto huyo alikiri kufanya kitendo hicho kwa madai ya kumkanya.

“Ni kweli nimempiga na kumchoma na moto ambapo nilikuwa nimeweka kisu kwenye moto kisha nikamchoma lakini nilikuwa najaribu tu kumuonya maana aliiba Sh 5,000 hivyo niliogopa baba yake angekuja kunigombeza kwamba nimetumia mimi hiyo pesa,” amesema mama huyo.

 

Alisema alifanya kitendo hicho katika hali ya kumkanya ndiyo akajaribu kumchoma lakini hakudhani kwamba atamuumiza na pia baada ya kugundua vidonda vikubwa alianza kumtibu kwa kumpaka dawa.

Kamanda wa polisi Mkoa wa Tanga, Edward Bukombe, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuongeza kuwa mama huyo tayari anashikiliwa na jeshi hilo.

 

Naye Diwani wa Kata ya Maweni, Joseph Colvas, ameitaka Jamii kushirikiana kwa pamoja kufichua vitendo vya kikatili wanavyofanyiwa watoto majumbani.

“Niwatake pia kina baba tuwe tunafuatilia watoto wetu majumbani si kuwaachia wanawake peke yao ili kuweza kujua matatizo wanayokumbana nayo watoto wanapokuwa nyumbani hasa kwa walezi wao,” amesema.

CREDIT: Mtanzania.

Rwanda,Burundi Zatajwa Kuongoza Wahamiaji haramu Nchini

Comments are closed.