Ukweli Kuhusu Koneksheni ya Tabu Mtingita
MIAKA mitatu iliyopita, aliibuka mwanamke mmoja, mtu mzima f’lani hivi kwenye mitandao ya kijamii hasa Instagram, akichekesha kwa lafudhi ya Kimakonde.
Muda mfupi baadaye, aligeuka gumzo kwa jina la Tabu Mtingita. Alipohojiwa na Gazeti la IJUMAA WIKIENDA kwa mara ya kwanza, mwanamke huyo alijitambulisha kwa jina halisi la Saimba Mtingita, huku akikanusha kuwa yeye si Mmakonde, bali ni Mndengereko (kutoka mkoani Pwani) isipokuwa alikulia kwa Wamakonde (mkoani Mtwara).
Kwa sasa Tabu ni mchekeshaji mwenye jina kubwa Bongo, amekuwa akilamba madili ya matangazo ya biashara kupitia fani yake hii.
Hivi karibuni kulisambaa tetesi na vipande vya video chafu iliyodaiwa ni ya mwanamama huyo ambapo wapenda mambo hayo, walikuwa wakiulizia namna ya kuipata (koneksheni).
Katikati ya tetesi hizo, Gazeti la IJUMAA WIKIENDA limekaa chini na Tabu ambaye amefunguka mengi likiwemo suala hilo la video chafu.
IJUMAA WIKIENDA: Tabu kwa sasa jina lako limekua kubwa kwenye tasnia ya vichekesho Bongo, nini siri ya mafanikio?
TABU: Siri kubwa ya mafanikio ni kuwa na heshima kwa kila mtu na kujituma
katika kazi. Mimi ninafanya uchekeshaji katika hali ya nidhamu, hasa kimavazi na kimatamshi.
IJUMAA WIKIENDA: Kabla ya kuingia kwenye uchekeshaji, ulikuwa unajihusisha na nini?
TABU: Mimi ni mwimbaji mzuri na nilikuwa ninaimba kwenye baadhi ya bendi mkoani Mtwara. Niliwahi kuimbia Bendi ya Bandari; yaani nilikuwa kama Luiza Mbutu (Mwimbaji na Mkurugenzi wa Twanga Pepeta), lakini baadaye niliona kwenye vichekesho kuna fursa.
IJUMAA WIKIENDA: Unapitia changamoto gani kwenye fani yako hii ya uchekeshaji?
TABU: Kumchekesha mtu si kazi rahisi, maana kila mtu anakuwa na mudi yake, hivyo hadi mtu acheke si kazi ndogo. Ninachokifanya ni kujitahidi kuwa mbunifu ili kazi yangu ipokelewe vizuri.
IJUMAA WIKIENDA: Kuna video ya ngono ambayo inasambaa mitandaoni ikidaiwa kuwa anayeonekana mule ni wewe, ukweli ni upi?
TABU: Katika changamoto zote nilizopitia kwenye maisha yangu, hii ndiyo changamoto kubwa. Jambo hili limenichafua mno, ukizingatia mimi ni mama mwenye familia na ninayeheshimika.
Ukweli ni kwamba, aliyefanya kitendo hicho si mimi na sijawahi kufikiria kufanya michezo kama hiyo.
Narudia tena, mimi ni mtu mzima, nina familia kwa maana ya mume na watoto, ndugu, jamaa na marafiki, wananiangalia na kuniheshimu. Kiukweli jambo hili limenifedhehesha sana
halijakuathiri kwenye kazi na madili ya ubalozi ambayo unayo?
TABU: Hapana, haijaniathiri kwa sababu watu wangu wanajua mimi ni mtu ninayejiheshimu na ninafanya kazi zangu kwa nidhamu.
IJUMAA WIKIENDA: Kwa upande wako, unawaambia nini wale waliohusika kukuchafua?
TABU: Wawe wanaangalia na watu wa kuwafanyia hivyo maana mimi sina tatizo na mtu. Sasa kwa nini nifanyiwe hivyo? Watu hawajui nimepitia changamoto nyingi kiasi gani kwenye maisha yangu hadi hapa nilipo, hivyo waniache hivihivi; yaani hapa nasikia uchungu maana roho inaniuma.
IJUMAA WIKIENDA: Pole Tabu, je, kwenye kazi yako hii ya uchekeshaji umepata mafanikio gani?
TABU: Kwanza kuwa Tabu Mtingita huyu ni mafanikio makubwa mno kwangu. Kumbuka nimekuambia nimepitia changamoto nyingi kwenye maisha yangu. Nashukuru nimepata ubalozi wa kampuni ya maziwa na kubwa zaidi ninamshukuru Mungu sasa hivi nina biashara zangu ambazo ninazisimamia na zinakwenda vizuri. Kingine nimeweza kumiliki hadi gari.
IJUMAA WIKIENDA: Je, nini kinafuata sasa ambacho mashabiki wako wakitegemee kutoka kwako?
TABU: Nimeandaa video zangu mwenyewe ndogondogo ambazo zitakuwa zinatumia dakika 15 mtandaoni na tayari nimeshaongea na runinga moja, zitaanza kuruka ‘soon’.
Makala: Happyness Masunga