Umoja wa Wazazi CCM Upanga Magharibi Ilivyowafariji Watoto Wanaoteseka na Tatizo la Moyo
Dar es Salaam: 9 Desemba 2022, Wanachama na viongozi wa CCM Kata ya Upanga Magharibi, katika kuazimisha siku ya Uhuru leo wao wameungana na kwenda kutoa misaada kwa watoto wanaoteseka na tatizo la moyo waliolazwa katika Taasisi ya Jakaya Kikwete iliyopo Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Upanga jijini.
Msafara huo uliongozwa na Katibu wa Wazazi Kata ya Upanga Magharibi, Baraka Bulembo na Katibu wa Elimu na Malezi wa kata hiyo, Amira Seif.
Msafara huo ulifika kwenye taasisi hiyo na kupokelewa na Muunguzi Kiongozi, Steven Charles ambaye aliwatembeza wadi mbalimbali za watoto hao na kuwapa misaada kadhaa.
Miongoni mwa misaada hiyo ni pamoja na sabuni, mafuta ya kupakaa, maji ya kunywa, pampas, dawa na vitu vingine.
Baada ya kugawa misaada hiyo, Mkuu wa Msafara huo, Baraka Bulembo amesema wameamua kuitumia siku ya kusherehekea Siku ya Uhuru kuwafariji watoto hao na kuwapa kidogo Mungu alichowajaalia.
Katibu wa Elimu na Malezi, Amira Seif amesema pamoja na mambo mengine wamefika kwa watoto hao ili kujionea changamoto zinazowakabili ili kama kuna mambo yaliyo ndani ya uwezo wao wawezi kuangalia jinsi ya kuwasaidia.
Akiwa wadini hapo Amira alionekana kuguswa na hali mtoto mchanga aliyekuwa akitibiwa wadini hapo bila bima na kuamua kujitolea pesa yake ili mtoto huyo akatiwe bima na kuwapunguzia mzigo ndugu waliokuwa wakihangaika kumtibia kwa pesa ya mfukoni.
Amira aliwaomba Wasamaria Wema wengine nao kuacha kutumia kipato walichojaaliwa na Mungu katika kufanya anasa bali watembelee maeneo kama hayo na kujaribu kupambania afya za wenzetu na Mungu atawabariki zaidi.
Hajra Msangi ambaye naye anatoka Jumuiya ya Wazazi Upanga Magharibi aliwaomba Wasamaria Wema wengine kujitokeza hospitalini hapo kuwapa faraja watoto hao na kuzishauri taasisi za bima kuzidi kutoa elimu ya bima ya afya maana inaonekana wengine hawana elimu hiyo na mpaka sasa wananchi wenye bima hiyo ni wachache sana.
Akitoa shukrani zake Muuguzi Kiongozi wa Wadi ya Watoto ya Jakaya Kikwete, Steven Charles aliushukuru ujio kwa kwenda kuwapa faraja watoto hao na kuwapelekea misaada hiyo haswa kwa wale ambao hawajiwezi kiuchumi.
Steven amesema kwenye wadi hiyo kuna wagonjwa wa aina tofauti wapo wenye uwezo na wasio na uwezo wa kuvipata kiurahisi vitu kama hivyo. HABARI/PICHA NA RICHARD BUKOS /GPL