The House of Favourite Newspapers

Umuhimu wa Nafaka Zisizokobolewa Mwilini

NAFAKA ni vyakula vyenye wanga ambayo tunahitaji kwa ajili ya nishati kuupatia mwili nguvu. Nafaka ambazo hazijakobolewa, kama vile mchele wa rangi ya kahawia (Brown rice) na ngano ambayo haijakobolewa, ni vyakula vyenye afya zaidi. Chagua unga ambao umetengenezwa kwa nafaka ambazo hazijakobolewa. Mchele mweupe na mahindi vikikobolewa huondoa kiini-tete na ganda la juu ambavyo vimesheheni virutubishi. Nafaka hizo hukobolewa ili bidhaa zake ziweze kukaa muda mrefu dukani bila kuharibika.

Lakini bila kiini-tete na ganda la juu za nafaka zilizokobolewa hubadilika na kutengeneza sukari haraka sana mwilini na zinaweza kusababisha sukari kwenye damu kupanda hadi kufikia viwango vya hatari. Jitahidi kuepuka nafaka zilizokobolewa.

KULA VYAKULA VYENYE NYUZINYUZI

Nyuzinyuzi (fibre) ni sehemu ngumu ya mimea, kama vile majani, mashina na mizizi. Nyuzinyuzi husaidia kupunguza kasi ya ufyonzwaji wa sukari kwenye damu. Hii husaidia kudhibiti kiwango cha sukari kwenye damu, kuukinga mwili na kuboresha umeng’enyaji wa chakula Vyakula vyenye nyuzinyuzi ni pamoja na mbogamboga, maharage au jamii ya mikunde kama vile choroko, njugumawe nk. na nafaka ambazo hazijakobolewa, matunda na mbegumbegu.

KUPATA NYUZINYUZI ZAIDI:

Baada ya kutwanga na kuchemshwa, ni salama kula majani ya muhogo (kisamvu). Ingawa watu wamezoea kula mizizi ya muhogo, majani yake yana nyuzinyuzi nyingi zaidi. Kula mboga za kijani mara kwa mara kadri uwezavyo. Tengeneza unga kutoka kwenye maharagwe kama ufanyavyo kwa soya. Kula wali au ubwabwa ambao haujakobolewa na nafaka zingine.

KULA VYAKULA VYENYE PROTINI

Ukichanganya na vyakula vingine vyenye afya, vyakula vya protini kama vile samaki, mayai, nyama, njugu na mbegumbegu haviongezi sukari kwenye damu na ni vizuri kwa wenye kisukari. Unashauriwa kula kiasi kidogo sana cha vyakula vilivyochakatwa sana na kufungashwa viwandani na kupunguza matumizi ya vinywaji vitamu na pombe.

Vyakula vilivyochakatwa na kufungashwa viwandani au kufungwa kwenye makopo huwa vinavutia sana. Kawaida ni rahisi kuvihifadhi na kuviandaa na ladha yake ni nzuri, lakini vyakula hivyo mara nyingi huwa na sukari nyingi, chumvi nyingi na viambato ambavyo siyo vizuri kwa afya.

Kama umechoka, una njaa, au umetingwa na msongo, vyakula vilivyofungashwa viwandani ni vigumu kuepukwa. Kama yalivyo madawa ya kulevya au sigara, vyakula hivyo, baada ya kula, hukufanya ujisikie vizuri kwa muda mfupi.

Baadaye sukari yake hutoweka na utaanza kujisikia vibaya hata kuliko mwanzo. Kila mtu kwenye familia tunamshauri kutokula vyakula hivyo au kupunguza sana matumizi yake. Vyakula vingi vilivyochakatwa hutumia mafuta yenye gharama nafuu lakini ambayo siyo salama kiafya ukilinganisha na mafuta yaliyotokana na mimea.

Vinywaji vilivyokolezwa sukari hasa ni vibaya kwa afya yako. Huwa vina kiwango kikubwa cha sukari na hupandisha kiwango cha sukari kwenye damu yako haraka.

Comments are closed.