The House of Favourite Newspapers

Unahakika uliyenaye ni wa ndoto zako? -3

HII ni mada itakayo-kusaidia kukuondoa kwenye giza na kukupa maarifa mapya kabla ya kuanzisha uhusiano lakini pia kujua aina ya uhusiano ulionao sasa. Swali kuu la mada yetu ni, una hakika uliyenaye ni wa ndoto zako? Leo tunahitimisha mada hii kwa kujenga hoja za msingi ambazo zitakufanya ufanye uamuzi sahihi baada ya kuelewa vema aina ya uhusiano uliopo.

TAZAMA MFANO HUU:

Utafiti mdogo unaonyesha kwamba, vijana wengi wanaokutana shuleni (sekondari) na kuanzisha uhusiano huwa hawafiki mbali. Ama mapenzi huishia njiani au mara baada ya kumaliza shule na kila mmoja kurudi nyumbani kwao.

Huu ni uhusiano wa kitoto wa kudanganyana zaidi ambao mwisho wake huwa si ndoa. Wapo ambao wameanza mapenzi tangu wakiwa shule na baadaye wakaoana lakini si zaidi ya asilimia tano! Hawa wana tofauti kidogo na wale wanaokutana vyuoni – ni walewale lakini wana nafuu kidogo, maana umri unakuwa umesogea kidogo (kuanzia miaka 22) hivyo kuweza kufanya uamuzi sahihi, lakini wengine wanaangushwa na wenzao.

Mfano: Hawa na Rajab wamekutana chuoni Singida na kuanzisha uhusiano. Rajab ametokea Tarime na Hawa Arusha. Kila mmoja alipotoka ana mpenzi wake. Wamejikuta wameanzisha uhusiano baada ya kuzoeana kwa kasi wakiwa chuoni.Katika uhusiano huo,  Hawa anazama mapenzini na kujikuta anampenda zaidi Rajab na kuwa tayari kuachana kabisa na Ramoza, lakini Rajab yeye anapoteza muda tu (anamfanya mpenzi wa kuzugia) akirudi Tarime anakutana na Maimuna wake! Huu ndiyo ukweli rafiki zangu.

HEBU SOMA HAPA

Wewe kijana uliyeko chuoni (hasa msichana) uwe makini na namna ya kuanzisha uhusiano. Wengi ni walaghai, wanatafuta hifadhi ya muda tu. Ni vyema kutumia hekima yako vizuri. Usikubali kuwa pumziko la mtu ambaye atakwenda kuoa mwanamke mwingine.

Kinachowaponza ni ngono, kuna sababu gani ya kuanza kufanya ngono mapema kama ni kweli ana mapenzi ya kweli? Akishakujua kuna nini tena? Anajiburudisha halafu mwisho wa siku anakutosa. Utaolewa na nani? Hili ni jambo la muhimu kulitafakari ukiwa ndani ya umri nilioueleza hapo juu. Wapo ambao wakish-avuka miaka 27 (hasa wasichana) wakiwa hawajaolewa, wanakuwa tayari kuolewa na yeyote atakayejitokeza kwa lengo la kujiondolea nuksi. Nani amekudanganya una nuksi? Tulia, jipange!

KUHUSU WAZAZI

Wazazi ni viunganishi muhimu katika ndoa za vijana wao lakini wakati mwingine huwa vikwazo au husababisha maisha mabovu kwa vijana wao kutokana na kuwachagulia wapenzi. Hili ni tatizo kubwa sana.

Kuna binti mmoja alilazimishwa na wazazi wake kuolewa na mwanaume ambaye yeye hakumpenda. Akaomba sana wazazi wake wasikilize hisia zake, hawakumuelewa. Akafunga ndoa kwa shingo upande, sasa hivi ni majuto! Majuto si kwake pekee, hata wazazi nao wanajuta. Kila wiki binti anarudi nyumbani, kisa amepigwa! Mwanaume ni mlevi kupindukia, kosa dogo tu anapiga! Mwanamke amegeuka ngoma.

Akikaa muda mrefu sana bila kupewa kipigo ni wiki tatu. Hivi ninavyoandika mada hii yupo nyumbani kwao baada ya kupewa kipigo na mume wake. Ni vyema wazazi wakajua kwamba dunia ya sasa imebadilika. Wawaachie vijana wao waamue wenyewe mambo yanayohusu ndoa. Wasiingilie. Ni vizuri pia vijana kushikilia msimamo, maana mwisho wa siku, anayekwenda kuishi na huyo mtu ni yeye mwenyewe.

Kuna watu wanahofia laana. Ndugu zangu, hakuna laana kwenye suala nyeti na la hiyari kama hilo. Kwenye muunganiko ulioagizwa na Mungu mwenyewe. Acha kujidanganya, heshimu hisia zako. Naamini kipo kitu umejifunza na sasa ni kazi yako kuchukua hatua. Wiki ijayo nitakuwa hapa katika mada nyingine, USIKOSE!

Comments are closed.