Unaweza Kutumia Msimu wa Sikukuu Kuwasha Upya Moto Kwenye Penzi Lako

RAFIKI, kwanza nimshukuru Mungu kwa kunifikisha leo na kusherehekea vyema Sikukuu ya Krismasi na sasa tunasubiri kuupokea Mwaka Mpya. Katikati ya sikukuu hizi, unaweza kuzitumia kuwasha upya moto wa hisia kwenye penzi lako.
Ukweli ni kwamba maisha ya mapenzi yamewatumbukia nyongo wengi. Kwa wengine yamekuwa machungu mfano wa shubiri. Jambo lililonishtua ni jinsi ndoa nyingi zilivyo hatarini kuvunjika.
Haya nayasema baada ya kushiriki usuluhishi wa ndoa kadhaa. Usuluhishi wa ndoa hizi ulikuwa na jambo moja linalofanana. Kwamba wanaume wengi huachana na wake zao kutokana na utofauti wa mambo chumbani.
Kuna wanaume wanaopenda wafanyiwe mambo f’lani na wake, kuna wengine hawataki mambo f’lani na kuna wengine waliogubikwa na masharti mengi.
Kuna muda ambao mke anaweza kukuwekea ngumu, hadi uone Dunia imekuinamia. Zile siku unaporudi nyumbani na kumkuta mke ameweka sura ya kazi. Yaani unakuta kafura, hazungumzi, hacheki, hakuangalii wala hataki kukusogelea.
Na wewe labda umejitayarisha, umetafuna njugu, pilipili na umekunywa supu ya samaki na damu inachemka. Unaweza ukajaribu mbinu zako hapo za kumchekesha labda au kumuuliza, lakini mambo yakashindikana. Utafanyaje?
Ni vyema kuelewa pale mkeo anapokuwa amepoteza hisia za mahaba. Na jinsi unavyoweza kuziwasha moto hisia hizo hadi mwenzio apagawe, tumia sikukuu hizi kutengeneza mambo upya.
Kwanza yaepuke yale mambo au vitendo vinavyoweza kumpunguzia hamu ya mapenzi. Wengine hupungukiwa hamu wanapokaribia siku za hedhi, wakiwa na mambo yanayowasumbua akili na wengine kama umeanza kurudi nyumbani usiku wa manane.
Kuna vile vijimambo vinavyomkirihisha na kumtia kichefuchefu, kama unanuka mdomo, kama jasho lako linatoa harufu kali ama kama una tabia ya kumvamia, kumpanda, kumaliza na kulala usingizi.
Lakini pia unaweza kujua hisia zake za mapenzi au hamu yake ya kuoshwa roho. Wapo akina kaka ambao anapoingia nyumbani tu, anajua kama leo mambo yatakuwa shwari. Unaweza kumkuta mkeo ameoga vizuri, amejiremba, ametandika vizuri kitanda na ananukia vizuri. Ujue hii ni dalili kwamba leo mkeo anakutaka, nawe pia usizubae.
Lakini kuna akina dada tunaweza kuwatunuku shahada kwa kuweka sura ya kazi. Kaka hapa itabidi uanze uchunguzi wa siri ili ujue kulikoni? Cha kufanya, kama mlikuwa na mazoea ya kuketi pamoja, basi siku utakayoanza uchunguzi, ukifika nyumbani, mwite aketi karibu yako na aketi upande wako wa kulia tayari kwa kuanza upelelezi.
Mfanyie kitu ambacho hujawahi kukifanya kama vile kumshika sehemu yoyote ambayo huna mazoea ya kumshika.
Akifurahia ujue kuna matumaini, lakini ukiona anachukia kitendo hicho na anajisogeza kutoka ulipo na kwenda pembeni kidogo, kaka yangu ujue una kazi ngumu mbele yako.
Kama mna watoto na ukiona anapenda sana kuwa karibu na wanawe kuliko kuwa na wewe, kaka anza kukaza mshipi.
Unapozungumza naye kama hapendi kukutanisha sana macho yenu na kukwepa kuangalia macho yako moja kwa moja nakupa pole.
Kama mkeo anapenda kusonya kila wakati mnapokuwa pamoja, anapenda kujadili mambo ya shari zaidi furaha na ukifanikiwa kuingia naye kitandani akaonekana kama anatimiza wajibu badala ya kufurahia rusha roho, kuna shida.
Ufahamu kabisa kwamba mwanamke anakuwa katika tabaka kuu tatu, kwanza anakuwa na mapenzi ya ugeni kisha anatafuta faraja yaani kumpa raha inayostahili, hasa ikizingatiwa kwamba ni wewe uliye karibu naye na unayestahili kumpa kila anachotaka na cha tatu anatakiwa awe na kitu cha kukukumbuka kila unapokuwa mbali naye.
Kwa leo ninaishia hapa, nakutakia Mwaka Mpya wenye mafanikio tele. Kwa maoni na ushauri wasiliana na mimi kwa WhatsApp; 0713 750 910.

