The House of Favourite Newspapers

UPUNGUFU NGUVU ZA KIUME MATOKEO YA KUPATA SARATANI YA TEZI DUME

Upungufu nguvu za kiume matokeo ya kupata saratani ya tezi Saratani ya tezi dume hutokea na kuathiri tezi dume yenye kazi ya kuzalisha manii ambazo nazo zina kazi ya kuhifadhi mbegu za kiume  ‘spermatozoa’ na kuzisafirisha zinapotoka.

tezi dume ni ndogo kama punje ya karanga, lakini inapopata matatizo hukuwa na huwa rahisi kupapasa au kuonekana kwenye vipimo kama ultrasound. Saratani ya tezi dume ina matokeo mawili, kwanza  ni kukua taratibu na pili ni kukua kwa kasi au kitaalam tunasema  ‘aggressive and can spread quickly’.

VIGEZO VYA KUPATA SARATANI YA TEZI DUME

Vipo vigezo vinne vinavyoweza kumfanya mtu apate saratani ya tezi dume. Kwanza ni umri mkubwa, mwanaume yeyote kuanzia umri wa miaka 45 yupo hatarini kupata saratani hii hivyo basi ukiona una umri huo au zaidi ya huo, basi ni vizuri ukawahi hospitalini kwa uchunguzi haraka, pili ni jamii ya Kiafrika huwa anapata saratani hii kirahisi na akipata hukua au husambaa haraka na kuleta madhara  makubwa.

Tatu ni kuwepo kwa saratani hii katika familia mfano baba, kaka, babu au watu wa karibu ambao walipata saratani hii basi na wewe ujue  upo hatarini kupata tatizo hili hapo baadaye. Historia ya uwepo wa saratani ya matiti kwa bibi, mama au wanawake wengine wa karibu katika familia kunachangia wewe mwanaume kupata saratani ya tezi dume. Unene kupita kiasi  ‘obesity’ ni sababu ya nne ya kupata saratani ya tezi dume na husambaa haraka sana na tiba yake huwa ngumu.

CHANZO CHA UGONJWA

Hakuna chanzo maalum  hadi sasa kinachosababisha saratani hii, chanzo kikuu ni mabadiliko yasiyo ya  kawaida ya seli au chembe hai zilizo ndani ya tezi dume. Mabadiliko haya yasiyo ya kawaida kitaalam tunaita  ‘mutations’ husababisha seli hizo zikue na kusambaa kwa kasi sana, hali hii hufanya seli zisizo za kawaida ziishi kwa muda mrefu wakati zile za kawaida zikifa zote, hapa ndipo sasa zile zisizo za kawaida huanza  kutengeneza uvimbe na seli hizo kusambaa katika viungo vya jirani na kwenda mbali zaidi mfano kwenye mapafu, mifupa na sehemu nyingine.

DALILI ZA UGONJWA

Mgonjwa mwenye tatizo hili la saratani ya tezi dume huwa na dalili hizi zote au mojawapo au baadhi yake. Mgonjwa hulalamika shida ya kutoa mkojo, kila akisukuma hautoki au unatoka kwa shida na wakati mwingine unatoka tu wenyewe. Hata kama ukisukuma mkojo hautoki kama ilivyokuwa siku za nyuma, yaani utatoka kwa matonematone, mgonjwa atalalamika kutoa manii zenye damu anaposhiriki tendo la ndoa. Dalili nyingine ni maumivu ya nyonga zote mbili kwa muda mrefu, maumivu ya mifupa, kiunoni, mapaja na magoti. Mwanaume pia hupata tatizo kubwa la upungufu wa nguvu za kiume mara apatapo tatizo hili.

athari za ugonjwa wa Saratani ya tezi dume ina athari kuu tatu, kwanza ni kama tulivyoona ni upungufu mkubwa wa nguvu za kiume ‘erectile dysfunction’ ambao husababishwa na saratani yenyewe au matibabu utakayopatiwa mfano kama ni upasuaji, mionzi au hata dawa za homoni, lakini matatizo haya yanatibika na unaweza kurudia nguvu za kiume kwa kiwango fulani. Athari ya pili ni kushindwa kudhibiti mkojo, unaweza kujikuta mkojo unatoka wenyewe bila ku– control au hautoki kabisa.

Tiba ya haraka ni kuwekewa mpira wa mkojo au catheter. Athari ya tatu ni kansa kusambaa, saratani hii huweza kusambaa na kushambulia kibofu cha mkojo au kusafiri na damu hadi kwenye mifupa hivyo ukajikuta mifupa inavunjika tu yenyewe.

KINGA YA SARATANI YA TEZI  DUME

Kula zaidi matunda na mbogamboga za majani, epuka vyakula vyenye mafuta. Tumia zaidi virutubisho vyenye vitamins na madini, fanya mazoezi mara kwa mara mazoezi ya

viungo kama kutembea au kukimbia au kuruka kamba husaidia kudhibiti  kuongezeka kiwango cha kichocheo cha PSA ambacho ndicho kinachohusiana na saratani ya tezi dume. Dhibiti uzito wako kwa kuangalia aina ya vyakula unavyokula na mazoezi. Ukifikisha umri wa miaka 45 na kuendelea tafuta daktari wako utakayemwamini awe anakupa ushauri na kupima tezi dume mara kwa mara.

UHUSiANO NA TENDO LA NDOA

Kwa mujibu wa Mtandao wa Webmed, upo uhusiano mkubwa wa ufanyaji wa tendo la ndoa na mwanaume kupata saratani ya tezi dume. Upo ushahidi unaochanganya mambo ya kushiriki na kutoshiriki tendo la ndoa. Katika utafiti unaoripotiwa ulishawahi kufanyika huko Marekani ambapo wanaume elfu thelathini walishirikishwa wale waliofanya tendo la ndoa mara nyingi na wakatoa manii zaidi ya mara ishirini na moja wana nafasi ndogo sana ya kupata saratani ya tezi dume tofauti na wale waliofanya tendo hili mara nne hadi saba kwa mwezi na wakatoa manii.

Kwa hivyo inashauriwa  ukifikisha umri kuanzia miaka 45 na kuendelea ili kupunguza nafasi ya kupata saratani ya tezi dume uwe unashiriki tendo la ndoa mara nyingi iwezekanavyo na mwenza wako, umri hauna kikomo katika suala hili kwa mwanaume na mwanamke labda kama kuna ugonjwa.

UPUNGUFU WA NGUVU ZA KIUME

Mwanaume hatakiwi kuwa na tatizo hili katika maisha yake, kinachotokea kadiri umri unaposogea ni uwezo wa kushiriki tendo hili unapungua na hii yote ni endapo mwili wako hauna stamina au nguvu za kutosha. Kutokuwa na nguvu za kiume kunasababishwa na matatizo ya kiafya kwa hiyo upungufu huu pia ukiendelea husababisha kutokea saratani ya tezi dume. Kwa hiyo ukiangalia kwa undani ni mambo yaliyo katika mtiririko mmpoja.

USHaUri Ili kuepuka matatizo haya yote ni kubadilisha mtindo wa maisha, kula vizuri, fanya mazoezi na pima afya yako mara kwa mara na shiriki tendo la ndoa mara kwa mara.

Comments are closed.