The House of Favourite Newspapers

UPUNGUFU WA NGUVU ZA KIUME, WANAWAKE WADAIWA KUHUSIKA

KESI ya wanaume kupungukiwa nguvu za kiume zimezidi kushika kasi huku tafiti zikionesha kuwa tatizo hilo linazidi kuongezeka kila uchwao.

Akizungumza na Ijumaa Wikienda hivi karibuni, mtaalam maarufu wa masuala ya kisaikolojia nchini Chris Mauki alisema: “Uchunguzi unaonesha kwamba kwa kiasi fulani wanawake wanachangia upungufu wa nguvu za kiume.

 

“Msingi wa nguvu za kiume umejengwa kwenye hisia ambazo hupatikana kwa mwanaume asiyekuwa na tatizo la kibailojia au kisaikolojia.

“Kama utamkuta mwanaume hana tatizo la kiafya na anakula vizuri lakini bado analalamikia upungufu wa nguvu za kiume ujue atakuwa na tatizo la kisaikolojia,” alisema Mauki.

 

Aliongeza kuwa, pamoja na kwamba masuala ya kisaikolojia ni mapana lakini kwa uchunguzi wake kupitia wanaume aliokutana nao na kuwashauri; amegundua kwa kiasi fulani wanawake wanachagia tatizo hili ambalo linawavunjia heshima baadhi ya wanaume.

 

WANAWAKE WANAVYOCHANGIA

Akifafanua jinsi mwanamke anavyoweza kusababisha mwanaume akapoteza nguvu zake za kiume, mwanasaikolojia huyo alisema:

“Unapozugumzia tatizo la upungufu wa nguvu za kiume wengi wanadhani ni tatizo la mwanaume mwenyewe; wakati si kweli, mwanamke naye anahusika katika hili.

 

“Kwa mfano ukikutana na mwanamke faragha ile unaanza tu kushiriki naye tendo yeye anaibuka na kukuambia ‘bwana mi naona unanichosha tu huwezi kazi’; unadhani nini kitatokea kama si hisia za mwanaume kupotea na kupoteza pia ujasiri?”

 

UCHUNGUZI UNASEMAJE?

Aidha, uchunguzi uliofanywa na mwandishi wetu kupitia ripoti za utafiti mbalimbali zilizofanywa kuhusu upungufu wa nguvu za kiume na mazungumzo kati yake na wanaume mbalimbali jijini Dar, wanaodai kuwa na tatizo hilo unaonesha yapo mambo kadhaa ambayo yanashibisha hoja ya mtaalamu Mauki na huchangia mwanaume kupoteza msisimko wa kimapenzi.

 

Miongoni mwa mambo hayo ni pamoja na baadhi ya wanawake kukosa ujuzi wa kuwaridhisha wanaume tofauti na mahitaji yao katika kushiriki tendo la ndoa kwa hamasa.

Aidha, hali ya mwanamke kutokuwa msafi wa mwili na mavazi huchangia kumpotezea mwanaume uwezo wa kushiriki tendo la ndoa, jambo ambalo likimtokea hufikiri kuwa ana tatizo la nguvu za kiume kumbe amekwazwa na hali ya uchafu wa mwanamke aliyekutana naye.

 

Jambo jingine ambalo linaweza kuchangia mwanaume akakosa hisia za kimapenzi ni hali ya kukutana na mwanamke aliyejaa lawama na tuhuma za kila aina kwa mpenzi wake; wengi huwaita wanawake wa jinsi hiyo kuwa ni wenye gubu.

Aidha hali ya usaliti wa wazi kwa mwanamke inatajwa kuwa inaweza kumsababishia mwanaume akapoteza hisia kwa mpenzi wake kwa sababu ya kuhisi thamani yake wanapewa wanaume wengine na hivyo kujikuta moyo wake ukisusa.

Matatizo haya yakichukua nafasi kubwa katika uhusiano wa kimapenzi huweza kumuathiri mwanaume kisaikolojia na kujikuta hawezi kufanya tendo la ndoa kwa ukamilifu.

 

MAKOSA MENGINE YA WANAWAKE

Aidha, makosa mengine wanayofanya wanawake na kusababisha hisia za wanaume kupotea ni pamoja na wao kutokuwa karibu na wapenzi wao.

Mengine ni kutowajibika ipasavyo kwa mahitaji ya wanaume na kutumia muda mwingi kufanya kazi za ulezi wa familia na za kuajiriwa jambo ambalo huwafanya wanaume kuhisi hawahitajiki na hivyo kupoteza msisimko wao wa kimapenzi.

 

Mambo mengine ambayo yanatajwa kuchangia upungufu wa nguvu za kiume ni hali ya wanawake wengi nyakati hizi kutojistiri maungo yao nyeti, mambo ya ngono kufanywa bila faragha tofauti na ilivyokuwa zamani.

 

DAKTARI ANASEMAJE?

Akizungumza na mwandishi wetu kwa njia ya simu, daktari maarufu nchini Godfrey Chale alisema ni vyema uchunguzi ukafanywa ili kubaini tatizo hili linalowasumbua baadhi ya wanaume.

“Juzi kuna utafiti ulitolewa kwamba asilimia 24 ya wanaume wa Kinondoni (jijini Dar es Salaam) wana upungufu wa nguvu za kiume.

 

“Nilijiuliza utafiti huo ulifanywa kwa njia gani na kuja na matokeo hayo? Katika kazi yangu nimekutana na kesi nyingi za wanaume wanaodai kuwa na upungufu wa nguvu za kiume.

“Wapo wanaoweza kukufuata na kukuambia wanahitaji dawa za kuongeza nguvu za kiume; si kwamba hawana hizo nguvu lakini wanataka kwenda kuwashughulikia zaidi wanawake wanaokwenda kukutana nao kingono.

 

“Sasa kumeza dawa ili kumshughulikia mwanamke kwa kumkomoa au vinginevyo huo si upungufu wa nguvu; na watu wa aina hiyo wakishazoea kumezameza hizo dawa hujikuta katika tatizo la kuhisi wana upungufu wa nguvu kumbe wameathirika kisaikolojia, ndiyo maana nimesema tufanye utafiti wa kitalaam tutafahamu tatizo na kulimaliza,” alisema Dk. Chale.

STORI: MWANDISHI WETU, DAR

Comments are closed.